Thursday, May 24, 2012

KWA NINI NCHI ZA ASIA MASHARIKI AU ASIA MASHARIKI YA MBALI ZIMETUPITA KI-MAENDELEO?

Na Africar T Kagema
Huu ni wakati muafaka; tunahitaji kufundishana juu ya nchi hizo za Asia Mashariki na ya Mbali (au mojawapo tu) zilizotuacha nyuma, ki-maendeleo.
Kusudi la makala haya ni kujaribu kukidhi haja ya kujaza ombwe linalozidi kuongezeka kutokana na makelele mengi ya kujilinganisha na nchi za Asia Mashariki na ya Mbali (au mojawapo ya nchi hizo) nikizingatia, kwa ujumla, vigezo au viungo-tosheleza vingine (zaidi ya elimu) katika mapishi yaliyokwamua nchi za Indonesia, Malaysia na Singapore na kuiacha Tanzania nyuma.

Tukizidi kujaliwa, nitachangia kwa kina mfano wa Kisiwa cha Singapore (Zanzibar ni kubwa) katika kujaribu kuelewa kwa nini Singapore imetuacha nyuma.
Macho … Asia Mashariki na ya Mbali, Elekeza!
Uduni wa elimu nchini Tanzania umezalisha umbumbumbu wa kutojua Kiingereza miongoni mwa vijana wetu kiasi cha kuathiri ajira kwao; hususan katika hoteli za utalii huko Kasikazini ya Tanzania.

Zaidi, uduni huo umezalisha umasikini mkubwa kiasi cha nchi yetu kuachwa nyuma sana na baadhi ya nchi zilizolingana kwa umaskini (na zilizojitawala wakati karibu mmoja) na Tanzania, yaani, Indonesia, Malaysia na Singapore. Leo hii zinatengeneza magari na makomputa na zinaingia kundi la nchi zilizoendelea.
Rais Benjamin W. Mkapa (wakati anaanza u-Rais) katika mkutano wake na wa-Tanzania nyumbani kwa Balozi Daudi N. Mwakawago (sasa marehemu) katika Mt. Vernon, New York, alishauri wa-Tanzania wageuze macho yao kuelekea huko Asia Mashariki na kuiga mifano ya ‘tigers’ hao katika jitihada za kuharakisha maendelo ya Tanzania.

Tanzania tayari imeiga baadhi ya mikwamuo ya nchi hizo. Miradi ya ujenzi wa viwanda vya ‘Special Economic Zones (SEZ)’ au ‘Special Export Processing Zones’ katika mikoa ya Arusha, Dar es Salaam, Kagera, Kigoma, Kilimanjaro, Manyara, Mtwara, Mwanza, Pwani, Shinyanga na Tanga ni mifano ya kutekeleza lengo la ‘Tanzania Mini-Tiger 2020’, kama ulivyo mfano wa sehemu ya Benjamin William Mkapa Special Economic Zone (BWM-SEZ), Mabibo, Dar es Salaam.
Matokeo-dhamiriwa (anticipatory results) ya ‘Special Economic Zones (SEZ)’ au ‘Special Export Processing Zones’ ni pamoja na kuongeza mauzo nje (utajiri), ajira na kumaliza umasikini (pengine, isomeke, kupunguza; sio rahisi kumaliza umasikini) ili kufikia lengo la ‘maisha bora’.

Ndoto ya kutaka kuiga nchi za Asia Mashariki pia imewakumba baadhi ya wana-siasa wa-Zanzibari wenye kutaka kuiondoa Zanzibar kutoka mabano ya uchumi wa Muungano na kuiendeleza, mithili ya Hong Kong, Dubai ama Singapore. Kwa mfano, katika hotuba ya Maridhiano na Mustakbali wa Zanzibar, 2010, mwana-siasa Seif Hamadi Shariff (Katibu Mkuu – CUF) anasikika na/au anasomeka (kwa kifupi) kuifanya Zanzibar kuwa ni Hong Kong ya Afrika:

“Binafsi naamini kuwa sasa ile ndoto yetu ya muda mrefu ya kuifanya Zanzibar kuwa ni Hong Kong ya Afrika Mashariki itaweza kutimia ndani ya muda mfupi kabisa. Naamini Wazanzibari wote… kuikwamua Zanzibar katika umasikini ambao hauna sababu ya kuwepo…Zanzibar ina utajiri mkubwa…inaweza kurudia nafasi yake ya kuwa kituo kikuu cha biashara na harakati za uchumi katika Afrika Mashariki na Bahari ya Hindi… itakuwa johari na siyo tena jeraha katika Afrika…Tusiruhusu kidudu mtu yeyote akaingia kati kuturudisha kule tulikotoka.” – (rejea: hakinaumma.wordpress.com/2010/01/23/maridhiano-na-mustakbali-wa-zanzibar/
Sio tu wana-siasa wetu wanaoota kuiga hayo ya maajabu ya kujikwamua kwa nchi za Asia Mashariki na ya Mbali. Wengi wetu pia tumepiga makelele sana (na miangwi yake imeenea milimani, mabondeni na kwenye tambarare za nchi yetu) kuitaka Tanzania yetu iendelee, kama nchi hizo (au mojawapo).

Kutokana na sababu sita hivi kubwa, naunga kwa mkono upande ujenzi wa ‘Special Economic Zones (SEZ)’ au ‘Special Export Processing Zones (SEPZ) zenye madhumuni ya kuifanyaTanzania yetu ijulikane kama ‘Tanzania Mini-Tiger 2020’:
Mosi, nachelea kidogo kutumia jina la ‘mini-tiger’ kwa Tanzania ya mwaka 2020; hatuna ‘tiger’ Tanzania! Badala yake ninapendekeza kuiita kwa kutumia msamiati wa ‘cheetah’ – mnyama wetu mwenye spidi kali! Tanzania ianze kama ‘a cheetah cub’ na itakapotimia umri wa kujikwamua hasa, iitwe, ‘a cheetah economy’. Pendekezo hili linahusu pia kila nchi za Afrika Mashariki-tegemewa itakayojikwamua; zote kwa pamoja ziitwe, ‘cheetah economies’.

Pili, hizi ‘Special Economic Zones (SEZ)’ au ‘Special Export Processing Zones (SEPZ)’ zenye kuwapa misahaha mingi tu ya kodi na kadhalika wawekezaji wa nje zinapunguza kodi ya mapato sana. Tatizo la upungufu wa kodi ya mapato lilibainika mbele ya Taasisi ya Fedha ya ki-Mataifa (IMF) – rejea: english.peopledaily.com.cn/200604/12/eng20060412_257859.html/
Tatu, viwanda vingine vinalazimika kutumia malighafi za nje, kama yalivyo baadhi ya masharti ya AGOA ya Amerika kwa Afrika kuhusu biashara ya nguo na kadhalika; tunabakia ni washonaji tu.

Nne, ndio viwanda vya namna hii vinaongeza ajira. Lakini vinatumikisha wafanyakazi wake mithili ya punda. Rejea, malalamiko ya wafanyakazi huko Fort Hall, Kenya, na soma baadaye Addidas na makampuni mengine ya huko Asia Mashariki na ya Mbali.

Tano, wawekezaji ni wa nje au wanatafuta waendeshaji kutoka nchi ambazo zina ujuzi zaidi ya wa-Tanzania. Kwa mfano, viwanda vingi vya ushonaji vinaajiri waendeshaji kutoka huko Asia Mashariki. Wawekezaji wakiisha kuchuma, huhama wakati mwingine bila ya kutoa ‘transfer of technology’ kwa wazawa (kama wazawa watakuwepo tayari), kama walivyofanya huko Thailand.
Sita, wakati mwingine kuhama au kukunja virago kunatokana na ufisadi wa wakubwa wazawa kudai % zao kabla ya kuwakubalia kuendelea upya na mikataba ya kuwekeza!

Tunapenda sana kuipima Tanzania yetu kwenye mizani moja na nchi za Asia Mashariki na ya Mbali; Tanzania inaonekana inapungua. Wakati mwingine tunaipima na nchi nyingine za Afrika, kwa mifano, Mauritius na Botswana, na kuonekana kuwa inapungua, pia.
Hivi karibuni, wa-Tanzania wengine wameanza kubaini kuwa nchi ya ujirani mwema ya Rwanda huenda nayo ikajikwamua na kuiacha Tanzania yetu mataani! Pengine, inabidi tujifunze kutoka Rwanda ya ujirani mwema!

Kwamba elimu inachangia katika kuleta maendeleo ya watu na vitu ni suala lisilo na malumbano. Lakini hakuna uwiano wa moja kwa moja baina ya elimu na maendeleo. Kwa kuwa kuna wasomi, kwahiyo kuna maendeleo!
Kwa mfano, miaka ya muongo wa 1980 sehemu moja ya Ukanda wa Ziwa Victoria, Afrika Mashariki (kwa wa-Jaluo wa Kenya) iliongoza kwa wasomi wengi wenye PhD kutoka vyuo vikuu vya Afrika na nchi za nje kwa kila maili mraba Kusini mwa Sahara. (Nafikiri mpaka leo hiyo sehemu bado inaongoza.) Lakini sehemu hiyo haikuongoza kwa maendeleo katika Bara la Afrika.

Tasnifu (thesis) ya makala haya inazingatia kuwa elimu ina mchango wa lazima (necessary) lakini si wa kutosheleza (not sufficient) katika kukwamua nchi kutoka dimbwi la umasikini; kuna viungo vingine tosheleza katika hayo mapishi-kwamuzi.
Inafaa tutoe elimu bora ili kuiwezesha Tanzania kushiriki kikamilifu na kushindana katika ulimwengu wa usasa, ikiwa ni pamoja, pengine, na kufanikisha hayo ya ndoto ya ‘maisha bora’. Lakini itabidi tuangalie pia viungo vingine tosheleza katika mapishi-kwamuzi ya nchi yetu.

Tanzania inahimizwa kuelekeza macho yake huko Asia Mashariki na ya Mbali. Kwa nini? Kwa sababu nchi hizo zimepiga eti hatua kubwa za maendeleo. Ndio. Lakini maendeleo hayo yametokana si kwa kuwekeza katika elimu bora tu; yameungwa zaidi na siasa/sera nyinginezo, kama ifuatavyo:
Nchi hizo zilifanikiwa kujikwamua kwa sababu ya mikakati na michakato ya hali halisi ya kila nchi (domestic starters), kwa upande mmoja, na jinsi zilivyosaidiwa na hali halisi ya kutoka nje (external starters), kwa upande mwingine.

Nchi hizo zilitawaliwa na u-dikiteta wa/na chama kimoja na kupaliliwa na nchi za ki-bepari za Ulaya Magharibi na Amerika ili kudhibiti u-Komunisti; serikali zake ziliongoza dira ya maendeleo; mikakati ya ubia wa ‘partnerships’ na ‘transfer of appropriate technologies’ kati ya nchi hizo na nchi tajiri za Ulaya Magharibi na Amerika; zilifuata siasa na sera za kujitegemea (self-reliance policies); hata biashara ya makasino, kamari, umalaya, na madawa ya kulevya yalichangia; ubia wa wawekezaji wazawa na makampuni ya nje uliwanyonya wafanyakazi katika viwanda vya ‘sweatshirts’ (ushonaji): zalisha nafuu lakini uza ghali; na kila mmoja alihimizwa kuchapa kazi.
Baadhi ya siri za ndani (domestic starters) na za nje (external starters) ‘zinatisha’ mbele ya Tanzania yenye kuamini demokrasia na mfumo wa vyama vingi vya siasa na yenye kulilia maadili mazuri dhidi ya ufisadi; biashara ya makasino, kamari, umalaya na madawa ya kulevya; u-dikiteta/chama kimoja cha siasa.

Nchi za Asia Mashariki na ya Mbali zote hazikulingana au hazikufuata mfumo sawa wa maendeleo. Kuna nchi zilizoitwa, ‘four tigers kwanza (Japani, Korea Kusini, Hong Kong na Singapore); zilizoitwa, ‘emerging tigers’ (Indonesia, Malaysia na Thailand); na iliyokuwa inajaribu, ikaitwa, ‘entigerment’ (Philippines).
Asia Mashariki kwanza zilipendelewa na nchi tajiri na ma-benki ya Amerika, baadhi ya Nchi za Ulaya Magharibi pamoja na Benki Kuu ya Dunia na Taasisi ya Fedha ya ki-Mataifa (International Monetary Fund). Kati ya mwaka 1965 na 1990 Benki Kuu ya Dunia ilianza kuyaita mafanikio ya nchi hizo, ‘East Asian Miracle’.

Uingereza ikawa ya kwanza kuzibatiza nchi nne za Asia Mashariki kwa jina la ‘Asian Tigers’: Hong Kong, Korea Kusini, Singapore na Taiwan. Ma-bepari wa London mwaka 1995 (wakiongozwa na Waziri wa Fedha wa Uingereza Sir Kenneth Clarke na Makamu wa Rais wa Nchi za Ulaya Sir Leon Brittan) walipanga mkakati wa kuhamasisha mfumo-kusudiwa kwa nchi hizo.
Mabepari hao mwaka 1996 walifanikiwa kumpata mweza wao Waziri Mkuu wa Singapore Goh Chok Tong (aliyemfuata Lee Kuan Yew Waziri Mkuu tangu uhuru) katika kuzindua mfumo-kusudiwa.

‘Emerging tigers” za Indonesia na Malaysia zilianza na ajira katika kilimo, kama Thailand pamoja na hiyo ya ‘entigered” (Philippines), ambayo ilianza kujikwamua wakati wa utawala wa Rais Fidel Ramos ikifadhiliwa na Amerika.
Mbali ya Indonesia, Malaysia na Singapore kuelea juu ya utajiri wa mafuta na gesi, faida yake iliendeleza sera za kujikwamua kati ya mwaka 1985-86. Singapore pia ni kisiwa kidogo sana (City State) ina bandari-ghala (entrĂªport) na uwanja wa ndege maarufu duniani kwa ajili ya biashara kubwa zinazopita mlango-bahari wa Malacca (sawa na Gibraltar, Istanbul na Panama) kati ya Bahari za Hindi na Pasifiki.

Kudhibiti Biashara Haramu na Tabia Zake
Biashara kubwa ya huko Asia Mashariki ya Mbali ilikuwa ya haramu (the illegal ‘black” economy) yenye faida kubwa: u-malaya, madawa ya kulevya, riba ya uajiri (labor export brokerage fees), magendo ya silaha, wizi wa mafuta, kamari, ma-kasino, bahati nasibu za njia za panya na kupiga kamari mipirani.
Kwa mifano, Singapore na Hongkong zilijengeka kama masoko makubwa ya kikoloni ya ki-fedha na dhidi ya biashara ya madawa ya kulevya chini ya China; ‘kufua fedha’ (money laundering): umalaya uliingiza mapato ya $17.7-20 bilioni; madawa ya kulevya $3.9 bilioni; riba ya uajiri (labor export brokerage fees) $2.4-3.2 bilioni; magendo ya silaha kati ya $512 milioni na $2.4 bilioni; wizi wa mafuta $334 bilioni; na kamari (ma-kasino, bahati nasibu za njia za panya na kupiga kamari mipirani $17.71-53.21 bilioni.

Malaysia ilijiepusha na balaa la kuanguka kwa uchumi kwa kufungua uchumi wa ma-kasino huko Labuan Island, mwaka 1990 ili kushindana na Hong Kong katika ‘money laundering’. Hata hivyo, ilipoteza $10 bilioni katika kumshinda ‘mega-speculator George Soros’.
Zaidi, Malayasia ilizidi kujenga ‘casino economy’ kwa kuwekeza huko Kambodia kwenye ma-kasino ya Sihanoukville, mabarabara, viwanja vya ndege na nishati. Shirika la Ekran lilijenga ma-kasino ya ‘offshore’ huko Davao.

Philippines mwaka 1995 ilifuata mkumbo wa Malaysia na kuwekeza katika Kisiwa cha Mindanao – kufuatia muafaka na wa-Islamu baada ya vita miaka zaidi ya 20. Philippines ilizindua mafao ya wafanyakazi, reli, nishati, bandari na viwanja vya ndege, na kufungulia wawekezaji ikiwa na kurejesha ugenini faida yote ya ‘joint-ventures’.
Baada ya Hong Kong kurudishwa kwa wa-China, wawekezaji walitoka Hong Kong) na kuwekeza huko Phillipines – kwa kaulimbiu, The Hongkongization of the Philippines. Leo hii kasino kubwa ni ile iliyojengwa kwenye uwanja wa zamani wa ndege za ki-vita wa Amerika, Clark Field, (the Las Vegas of Asia) pamoja na viwanja vitano vya ma-kasino-tamasha ya Disney.

Ubia: Serikali/Sekta Binafsi
Siri nyingine zilitokana na serikali kuwekeza katika elimu bora na tosheleza kukidhi ajira na kuuzika kwa wabunifu mbele ya wawekezaji wa ndani (domestic entrepreneus); uzalendo wa kuchapakazi, mishahara bila matabaka na akiba.

Serikali zilifuata na zilidumisha sera zenye tija (pragmatism) kwa nchi na kukubali kuoanisha sera hizo kwa mahitaji ya nchi (eclecticism); mishahara ya wafanyakazi wa serikali iliyolingana karibu sawa sekta binafsi; faida ya matunda ya uhuru kwa wote bila kubagua rangi au miji/vijijini; na kujiwekea akiba binafsi na taifa.

Kulikuwepo pia na upendeleo mkubwa kutoka kwa ma-bepari. Ikifuatia nyayo za Japani, Uingereza ilijaribu ‘to recolonize’ Asia Mashariki ya Mbali kupitia kuwekeza katika taasisi na shughuli za fedha (financial control): mabenki ya biashara na bima ya maisha. Iliwekeza huko Indonesia baada ya kufunga biashara huko Singapore na Hong Kong.

Ubia wa serikali na sekta binafsi ulivuta wawekezaji wa nje. Lakini serikali haikujiondoa katika kuongoza dira ya maendeleo kwa kuweka malengo na mipango ya taifa. Ubia huo uliwezesha kuhamisha ujuzi na uzalishaji (transfer of information and appropriate technologies).
Shirika la Mafuta la Malaysia (Petronas) ni mfano mzuri wa (‘transfer of technology’). Shirika hili liliundwa na Waziri Mkuu Mahathir Mohamad kwa kukopa mfano wa Indonesia na kujenga Heavy Industrial Corporation of Malaysia (HICOM).

Uongozi wa serikali za nchi hizo uliingilia kati uzalishaji wa miradi ya maendeleo iliyoendana na wakati. Hili ni la muhimu kuzingatia. Historia ya nchi nyingi zilizoendelea kwa kasi inaonyesha miingilio ya serikali zake katika kuongoza mikakati ya maendeleo.
Kwa mfano, ukoloni ulifuata sera za kusetri kwa nguvu zote wawekezaji binafsi: Uhispania, Ureno, Italia, Ufaransa, Ujerumani, Ubelgiji na Uingereza tangu enzi za ‘ugunduzi’ (the age of overseas discoveries) na wakati wa ukoloni.

Mfano wa Amerika pia unafuata huo wa Nchi za Ulaya Magharibi. Mbali ya utajiri wake kukuzwa na kuendelezwa na mfumo-unyama wa utumwa, serikali ilieneza ukoloni wake ikilinda wawekezaji na wakazi kuelekea pande za Amerika (kusini na magharibi), Visiwa vya Pasifiki, Panama City – wakati waujenzi wa Mfereji wa Panama – hadi huko Hawaii na Alaska.
Urusi nayo ilifanya hivyo hivyo, kama serikali ya Amerika. Serikali ilieneza ukoloni wake huko Ulaya Mashariki na, baadaye, kujenga himaya ya Soyuz Sovietskikh Sotsialisticheskikh Respublik (Union of Soviet Socialist Republics) au USSR, kwa kifupi.

Serikali ya Nazi-Ujerumani iliingilia kati uchumi wa nchi hiyo kwa ubia kati ya serikali na sekta binfasi (cartels) kiasi cha kuwa na uchumi uliokuwa ukikua kwa ari, nguvu na kasi sana kushinda uchumi wa nchi yeyote duniani wakati huo.
Huu ndio mchango mkubwa wa siri ya kujikwamua kwa nchi za China, India, Brazil na (sasa) Vietnam!

Hazikufungwa na Itikadi Moja
Nchi hizo hazikufuata itikadi ya aina moja (a single-ism); chache (Hong Kong na Singapore) zilisaidiwa na nafasi ya jiografia. Nchi hizo pia hazikuendelea kwa spidi moja. Ndio kusema kulizaliwa ‘tigers’ wengi sio mmoja. Sera za serikali ziliendana na wakati (fluidity in the policies) na zilijenga u-hakika (generated confidence) miongoni mwa wadau wote wa uchumi.

Hong Kong ilifuata sekta binafsi iliyojipangia mipango na miradi ya maendeleo bila serikali kuingilia au kupanga cha kuzalisha.
Indonesia, Malaysia na Singapore serikali zake zilikuwa na ubia na sekta binafsi na kuunda timu ya mipango na miradi ya maendeleo (zikiiga mfano wa Korea Kusini) na mabenki nchini yalishirikiana na wazalishaji na kupendelewa na Uingereza, Amerika na Benki Kuu ya Dunia ili zicheze mchezo na ‘the big boys’.

Taiwan ilikuwa na sera za bora liende – mchakato mchanganyiko; ilifanikiwa kuwa kiwanda cha dunia kilichozalisha bidhaa kwa kuongezea thamani (value-added products).
Nchi nyinginezo ziliiga mfano huu wa viwanda vidogo vidogo kwa ajili ya kulisha viwanda mama (mother plants) vyenye uwezo wa kubuni na kuongeza uzuri na thamani ya vizalishavyo, kuongeza maarifa katika ajira na kutengeneza mashini bora.

Kujitegemea, Kujinyima, Kuweka Akiba
Zaidi, nchi hizo pia zilijikwamua kwa matokeo ya siasa na sera za kujitegemea (self-reliance and import substitutions policy) katika kutoa elimu na uzalishaji/ulaji wa vya nchini kuliko kununua vya usasa kutoka nchi tajiri na kuuzwa na mawakala-uchwara. Sera hizi zilisaidia kuzuia faida isitoroshewe nchi za nje bali itunzwe nchini. Wananchi walijinyima kununua vya anasa kutoka nje; sawa na kijito kunywesha mto, kunywesha bahari.
Nchi hizo pia zilijinyima na kuweka akiba kwa kwa upande wa wananchi na serikali zao na kuwekeza katika mipango ya maendeleo – siri kubwa ya maendeleo. Wananchi walijiwekea akiba bila kufuja pesa zao kwa kukimbilia kununua vya usasa kutoka nje. Mishahara ya wafanyakazi ilipunguzwa bila kuwafukuza ili kulinda ajira kwa wote.

Kutokana na kuweka akiba, riba ya mabenki ilikuwa juu; wafanayakazi waliweka mapesa yao ma-benkini. Hii ilisaidia kuhimili uwekezaji kutoka ndani kuliko kutegemea wafadhili kutoka nchi za nje au kutembeza mabakuli ya mikopo nchi na kulipa riba kubwa.
Hata hivyo, kutokana na kupendelewa na wakubwa, nchi nyingi zilitembeza mabakuli mbele ya IMF na kupewa ‘grants’ sio mikopo.

Kuna nchi zilizoweza kujinyima kiasi cha 30-40% (GDP). Uzalishaji ulikua sana na kuzalisha vingi vya kuuzwa nchi za nje kwa faida kubwa. Thamani ya pesa haikupanda sana ili zizalishe kwa u-rahisi, ziuze nchi za nje ghali, uchumi uzidi kukua, na kuacha kuwa mawakala wa vya nje.
Kwa mfano, Singapore ili kuwawezesha wananchi wake kutofuja utajiri wao, serikali ilihimiza kutunza zaidi ya 20% ya GNP. Ni kutokana na sera hii Singapore ilifanikiwa kutunza karibu 42% ya GNP. Wananchi walihimizwa kununua vya nyumbani kuliko kununua vya kutoka nje.

Pesa zilizohifadhiwa zilitumika katika uwekezaji wa vitu, mashini, mali, vifaa, miundombinu, mabarabara, bandari na viwanja vya ndege, na katika kutandaza njia za mawasialiano (broadband infrastructure), elimu, afya, kukidhi bidhaa na vifaa-chakavu, ufanisi wa wafanyakazi ili kuweza kushindana na wengine bila kudororesha uchumi.
Utandawazi ulipoanza kurindima, nchi hizi zilijikuta zina mapesa ya ziada kuliko miaka ya nyuma. Mapesa hayo yalisaidia kukuza ajira na kuzalisha zaidi. Hivyo, toka mwaka 1960 hadi 2000, nchi hizi kwa miaka 40 ziliweza kujikwamua kutoka umasikini.

Serikali na sekta binafsi zilikuwa macho katika kupanga na kuchagua ni wapi pa kuwekeza kupitia mipango ya taifa ya maendeleo.
Malaysia imeboresha miundombinu, na kuufanya mji mkuu wa Kuala Lumpur mji wa kisasa unaojitegemea: makazi, maofisi, na burudani – mji uliounganishwa na miundo mbinu ya reli na mji wa serikali huko Putrajaya.

Mitandao ya mabarabara imesaidia sana kuunganisha viwanda na bandari na viwanja vya ndege ili kurahisisha usafirishaji wa bidhaa kati ya Kuala Lumpur-Bangkok-Kuala Lumpur kwa kutumia makontena ya Asean Rail Express (ARX). Na njia kuu ya Trans-Asia Rail Link kuunganisha nchi za Singapore, Vietnam, Cambodia, Laos na Myanmar hadi huko Kunming nchini China.
Malaysia pia imekuza bandari zake ili kuchuma kutokana na biashara za ki-mataifa: Penang, Klang, Johor, Tanjung Pelepas, Kuantan na Kemaman (Jimbo la Malaysia) na Bintulu (Jimbo la Sarawak).

Lakini haikuishia kujenga bandari hizo tu; imebidi kuimarisha na kuboresha huduma zake. leo hii bandari hizo ni ‘free-zones’ zinazovutia biashara ya majini.
Malaysia pia inajivuna shirika lake la ndege na viwanja vya ndege vyenye hadhi ya ki-mataifa kwa ajili ya abiria na mizigo: Kuala Lumpur, Penang na Langkawi (Jimbo la Malaysia), Kota Kinabalu (Jimbo la Sabah) na Kuching (Jimbo la Sarawak).

Kwa kushirikiana na sekta binafsi, serikali ya Malaysia imewekeza katika kuboresha viwanda vyake 18 vya ‘Free Industrial Zones (FIZs’) vilivyosambazwa nchini na kuunganishwa na miundombinu na huduma nyinginezo: barabara, umeme, na maji, na mawasiliano.
Viwanda hivyo vilidhamiria kuzalisha bidhaa za kuuzwa nje na kuingiza pembejeo bila malipo ya forodha: mali ghafi, vipuri, mashini na vifaa muhimu.

Kuna pia sehemu zimetengwa (specialised parks) kwa ajili ya viwanda maalum: viwanda vya teknolojia huko Bukit Jalil, Kuala Lumpur na Kulim huko jimbo la Kedah, ikiwa ni pamoja na kubuni miradi ya maduka, hospitali na burudani.
Malaysia imeboresha sana miundo ya ‘hi-tech telecommunications’ ya ki-‘digital’ na ‘fibre optics’ (bandwidth, medium and high-end technologies: IDSL, IP, VPN na ATM) na matumizi mengine ya satellites (FLAG, SE-MA-WE, APCN, China-US, Japanese-US, Measat na Intelsat) ili kuharakisha mchakato wa mawasiliano.

Chama Kimoja, u-Dikiteta, u-Komunisti, Kuzawadi Dhuluma
Kila nchi (kutoka Korea Kusini, kupitia Taiwan, hadi Indonesia) iliongozwa na u-dikiteta na chama kimoja! Nchi za ma-bepari zilinyamaza kimya; hazikuhubiri injili ya demokrasia na heshima ya haki za binadamu! Nchi hizo zilitawaliwa ki-babe au ki-dikteta na maisha ya wananchi kudhibitiwa ki-‘nanny’ (yaya-mlezi mkali) – amani yenyewe ilijengeka kwa nidhamu ya woga, ki-jeshi jeshi.

Nidhamu kali ilisaidia kuleta amani (political stability) na kusetri uwekezaji. Kwa mfano, ungekamatwa ukitema ulimbo wa ‘chewing gum’ huko Singapore au kuchafua mazingira, ungetozwa faini au kuchapwa viboko.
Nchi zenye vyama vingi, chama-tawala kilicholeta uhuru kiliendelea kushika madaraka kana kwamba ni nchi ya chama kimoja, kwa mfano, huko Taiwani na Singapore.

Demokrasia na utawala bora (kama tukiondoa nchi ya Japani) ulikuwa ni utata mtupu; serikali zilihujumu haki za binadamu na huku zikishirikiana na serikali za nchi za ma-bepari kutaka kujenga ngome za kudhibiti kuenea kwa u-Komunisti.
Sera-ongoza za mambo ya ndani na nje za nchi hizo zilioana dhidi ya kulinda wawekezaji, mitaji ya nchi za Magharibi, ikiwa ni pamoja na kudhibiti kuenea kwa u-Komunisti (to contain communism) bila kujali haki za binadamu.

Maslahi ya ki-amani, ki-usalama na ki-uchumi ya Nchi za Magharibi wakati wa tawala za vyama vya siasa vya ki-hifadhina (conservative) huwa hayajali cha haki za binadamu. Wakubwa wakikupenda hata ukiwa ni dikteta, watakusetri! Ninatoa mfano wa hivi karibuni.
Kwenye mahojiano tarehe 19 January 2011 kati ya Waziri mstaafu wa Mambo ya Nchi za Nje na Mshauri Mkuu wa Usalama wa Taifa (Amerika) Henry Alfred Kissinger (m-Jerumani/m-Amerika) akihojiwa na Charlie Ross (Public Broadcasting Corporation, Channel Thirteen), kuhusu masuala mbalimbali ya uhusuano kati ya Amerika na China, kufuatia ujio wa ugeni wa Rais Hu Jintao wa China nchini Amerika, Kissinger alitamka bayana kuwa maisha au utamaduni wa ki-Magharibi (maslahi yao katika nchi za kigeni) ni tunu au azizi kushinda utamaduni mwingine duniani. Kwahiyo, Kissinger hataki kuiona China ikizipiku nchi za Ulaya Magharibi na Amerika.

Mpaka sasa China inaendelea kujikwamua na kuogopwa kwamba huenda baada ya miaka 25 itashika kilele cha ubabe duniani.
Hao ma-bepari wakubwa, wakiongozwa na Amerika, Uingereza, Benki Kuu ya Dunia na Taasisi ya Fedha ya ki-Mataifa, walipendelea nchi hizo kuwa tunu au vito (economic showcases) mbele ya nchi za u-Komunisti: China, Korea Kasikazini, Mymmar, Kambodia, Laos na Vietnam.

Wakati wa enzi za uhasama wa ‘Vita Baridi’, Nchi za Magharibi zilionesha upendeleo mkubwa kwa kuzikinga nchi hizo za Asia Mashariki na ya Mbali dhidi ya mwingilio na kuenea kwa u-Komunisti. Zilizawadishwa sana wakati wa tawala za mkondo wa kulia za Waziri Mkuu wa Uingereza Margaret Thatcher na Rais Ronald Reagan wa Amerika.
Zaidi, Balozi wa Amerika Paul Dundes Wolfowitz huko Indonesia hakutaka kukutana na wanaharakati wa haki za binadamu ili kujadili jinsi serikali ya Rais General Haji Mohammad Suharto (Soeharto) ilivyokuwa ikihujumu haki hizo.

Wakati wa enzi za Rais Ronald Reagan, Balozi Wolfowitz alisukuma suala la demokrasia na haki za binadamu ukumbi wa nyuma kuhusu uhusiano kati ya Amerika na Indonesia. Ziara ya Rais Reagan iliyobatizwa, ‘The Winds of Freedom Tour’, Balozi Wolfowitz hakupenda waandishi wa habari wa Amerika na Australia waalikwe wasije wakamwaibisha mwenyeji wao mbele ya Rais Reagan. Alipendekeza masuala ya uchumi tu ndio yaletwe mbele ya meza kati ya ma-Rais hao wawili.
Rais Suharto na Waziri wa Teknolojia B.J. Habibie walizawadiwa kuzindua sera ya viwanda mkakati (strategic industries) katika viwanda vinane kwa matumizi ya kijeshi na kiraia.

Korea Kusini na Taiwan zote zina historia karibu sawa na hiyo ya Indonesia katika kuhujumu haki za binadamu na kudumaza demokrasia. Taiwan ilipendelewa sana dhidi ya u-Komunisti wa ‘panda’ (China). Taiwan iling’aa wakati China (yenye wingi wa watu duniani) ikikosa maendeleo ya vitu na huduma.
Korea Kusini ilikingwa na kupambwa (a show case) na wakubwa dhidi ya m-Komunisti Korea Kasikazini – nchi ya siasa ya ‘juche’ – kujitegemea!

Serikali ya Indonesia (sawa na South Korea na Taiwan) ilijenga muundo wa maendeleo ki-muhula. Na huku ikitawaliwa kwa u-dikteta wenye kuhujumu haki za binadamu na kudumaza demokrasia eti kulinda haki za ‘constitutional liberties’ kupitia ubepari: ubinafsi (individual good) ulisheheni dhidi ya umma (common good).
Pamoja na nchi ya Indonesia kuua watu wengi nchini humo enzi za Rais Gerard Ford mwaka 1975, ilishambulia na kuua wananchi wa Timori Mashariki eti kwa kupinga u-Komunisti. Zaidi, ilitumikisha wafanyakazi kwa bei duni chini ya u-dikiteta wa mabuti ya viongozi wana-jeshi na chini ya tawala za chama kimoja!

Unyonyaji, Sweatshops, Economic Processing Zones, Uporaji wa Maliasili
Mvuto mwingine ulikuwa unyonyaji katika ‘sweatshops’ kwa vibarua wasio na elimu na wenye kulipwa kiduchu (faida kwa wawekezaji) kufuatia kuanguka kwa Latin Amerika ya Mexico. Wafanyakazi hao walilipwa kwa kumaliza ‘ngwe’ ya kazi waliyopewa, kwa mfano, kushona mashati 50 kwa siku.

Zaidi, kulikuwepo na hali ya unyonyaji wa maliasili (misitu, mafuta na madini).
Msomaji, pengine utakumbuka kisa cha wawekezaji wa Amerika, Adiddas, waliotuhumiwa sana kwa kuwatumikisha wananchi wa Indonesia na kuwalipa kiduchu.

Mstaafu Balozi wa Amerika Umoja wa Mataifa Andrew Young (enzi za Rais Jimmy Carter) alitumwa na makampuni ya Amerika yenye viwanda nchini Indonesia kujaribu kutoa ripoti za hujuma hizo. Ripoti ya Balozi Young ilishangaza wengi: alikataa kuwepo kwa hujuma hizo!
Mstaaafu Balozi Andrew Young leo hii ni mmoja wa wawakilishi wa makampuni ya Amerika yanayopora rasilimali za Bara la Afrika, ikiwamo kampuni ya madini ya Barrick nchini Tanzania. Ni mshiriki sana katika Mikutano ya Sullivan; alikuja kwenye Mkutano wa Sullivan Arusha!

Tunu Kuitwa ‘Tiger’
Msomaji, jina la ‘tiger’ linavuta na limeanza kuvuka mipaka ya uchumi na kuingilia uga wa elimu. Kwa mfano, sasa hivi Amerika kuna malumbano kuhusu hoja ya Prof. Amy Chua (a John M. Duff, Jr. Professor of Law at Yale Law School) – mama wa ki-China na mumewe mzungu wa ki-Amerika).
Prof. Chua anatetea akina mama wa ki-China kwa kujikita kwao katika mikakati na mapambano ya kulea, kufunda na kuwasaidia watoto wao wafaulu maishani, ikiwa ni pamoja na utii kwa wazazi na katika mashindano ya elimu mashuleni, bila kudekezwa, kama walivyo watoto wa Amerika.

Kitabu chake (The Battle Hymn of the Tiger Mother) kinafaa kusomwa kwa malinganisho (comparative purposes). Katika mada tofauti ya ‘Why Chinese Mothers Are Superior’ (tafsiri yangu – ‘Kwa Nini Mama wa ki-China ni Mahiri’) katika malezi ya watoto wao, Prof. Chua anajaribu kueleza siri ya kufanikiwa kwa watoto wake katika hisibati na muziki.
Kuna wenye kuwapigia debe akina mama-wazazi wa ki-China na kuwabatiza kwa jina la ‘Tiger Mothers’. Wataalam wengine wa taaluma ya elimu wanaanza kuamini kuwa huenda wa-Asia wana 1Q ya juu. Dai hili halina ukweli; ufaulu huo unachangiwa sana na mila za mashindano, kulingana na dhana ya Confucianism.

Kuna wa-Ulaya/Amerika ambao hupenda sana kula maini ya bata. Baadhi ya wafuga-bata wa Amerika, kwa mfano, wanamlazimisha bata kula chakula kingi hata kama ameshiba; chakula husukumizwa kooni kwa mashini ili bata aweze kujenga ini kubwa; kwani ini kubwa, pesa nyingi.
Hoja ya Prof. Chua imepokelewa kwa hisia tofauti. Wengine, wanamkosoa kwa kulea watoto wake, kulingana na dhana-tata ya ‘tabula rasa’ na kuwalazimisha kwa nguvu ‘wale chakula’ cha elimu, kama hao bata, ili waongoze madarasani na mashuleni! Wanaofaulu, hufanya vizuri maishani.

Lakini kushinikizwa huko hakuwaletei furaha maishani. Zaidi, watoto wengine (kwa kushinikizwa na wazazi wao) hujiua kama hawafanikiwi. Huko China na Korea Kusini kuna idadi kubwa ya vifo vya kujiua miongoni mwa vijana wa kati ya miaka 15 na 25!
Wanafunzi wa ki-Asia ni wengi sana na wanazidi kung’aa kwenye vyuo vikuu vya Amerika, hasa wa kutoka China na India. Zaidi, wakitahiniwa, ki-mataifa, wanafunzi wa huko Asia (na watoto wenye asili ya ki-Asia walioko, kwa mfano Amerika), wanafanya vizuri kuliko watoto wa kutoka kwingineko.

Hii inalifanya taifa la Amerika kujiuliza kwa nini linashika nafasi karibu ya nane katika masomo ya hisibati na sayansi!
Nimeingilia hili la ‘mashindano’ kushadadia hoja kuwa nchi tunazozizungumzia (hasa zenye watu wa asili ya ki-China na wenye kufuata dhana ya Confucianism) zilikumbatia kwa dhati kuchapakazi kwa mashindano.

Kwa mfano, kuna kisa cha Waziri Mkuu wa Singapore kuchapa kazi kiasi cha kukosa usingizi na mkewe (daktari) kumpa vidonge vya usingizi. Kuna siku alipokea ugeni kutoka kwa Malkia wa Uingereza na huku akiwa amelazwa hospitalini.
Tuzungumzia mfano wa Singapore katika juhudi yetu ya kuangalia kwa u-karibu na u-ndani kwa nini kisiwa hiki (kisicho na maliasili na kinachoagiza mchanga wa kujengea kutoka nje) kimeiacha Tanzania yetu mataani.

Singapore (The City of Lions) ipo kwenye Ukanda wa Joto wa Ikweta wenye joto na ufukutu mkali. Sehemu hiyo iko ki-mkakati (strategically) kwa usafiri wa majini kwenye Mlangobahari wa Malacca kutoka na kuingia Bahari ya Hindi, Bahari ya China Kusini, Bara la Australasia (Asia ya Mbali, Australia na New Zealand) na ina uwanja wa ndege mkubwa kwa usafiri wa angani.
Singapore, ‘chunusi kwenye uso wa Malaysia’, ina eneo dogo sana (kilomita-mraba 646 sawa na eneo la Jiji la Chicago, Amerika). Idadi ya watu haifikii milioni tano, ambao wamejigawa ki-uzawa; yaani, wa-Hindi, wa-Malay na wa-China. Zaidi, wamejigawa ki-dini; yaani, wa-Islamu na wa-Budha. Masuala ya siasa, ubaguzi wa rangi au dini hayaruhusiwi kuwa viini-zungumziwa na wasanii.

Kisiwa cha Singapore kilianza kama kijiji cha wavuvi wachache. Kilijaa mabwawa ya mbu wengi wenye kueneza ugonjwa wa malaria. Bandari na mandhari ya ufukwe wake kulijaa mitumbwi (sampans na junks). Walevi wa madawa ya ‘opium’ walijaa kwenye sehemu walikoishi jamii ya wa-China, ambao walikuwa wakichungulia madirishani na huku wamewaka chakari, mbali ya wapigakamari na kusheheni biashara ya u-malaya na u-shoga (changudoa).
Licha ya sifa hizo mbaya, Kisiwa cha Singapore kilikuwa kikishindaniwa kati ya Uingereza na China kutokana na jiografia yake. Waingereza walikitawala kwa muda wa miaka 149 kwa lengo la kukifanya mahali pa biashara na maghala/soko makubwa (commercial emporium), kama Hongkong, kwa masoko makubwa ya kikoloni ya ki-fedha na dhidi ya biashara ya madawa ya kulevya chini ya China.

Mwaka 1963 kilijitawala chini ya Muungano wa Malaya na Majimbo ya Sabah na Sarawak. Lakini Mungano ulivunjika 1965 kutokana na wa-China na wa-Malaysia kugombana. Vyuo vikuu vilijaa wasomi wa mkono wa kushoto; ma-Komunisti waliiingilia vyama vya wafanyakazi; na haikuwa na jeshi la ulinzi. Haikuwa na maliasili na eneo la kuzidi kupanuka; mji mchafu wa kunuka; mifereji ya maji machafu na taka kila mahali; na ajira haba.
Zaidi, ilikuwa inaagiza maji na chakula kutoka nje ili kusaidia lishe nchini ingawa ilikuwa na nguruwe, matunda na mboga; majitaka yalinuka kila mahali; na ajira haba sana kiasi cha 14%; na wenye manywele marefu (hippies) kutapakaa kila mahali.

Serikali (Waziri Mkuu) Yauvalia Njuga u-Masikini
Kujikwamua kwa Singapore kunalingana na methali ya wa-kuria: “Inyanyi ilatangata Ubukama.” (Tafsiri: Sumbuka (Henya) au taabu kwanza; ufalme uko (raha iko) mbele.”)
Singapore ilijiuliza maswali mazito: Singapore inaishi katika ulimwengu wa hali gani? Singapore imetoka, iko na inakwenda wapi? Singapore itilie mkazo mafunzo gani mashuleni ili kuweza kufanikisha ndoto ya maisha bora kwa wananchi wake?

Kutokana na jiografia ya Singapore, Waziri Mkuu wa kwanza Lee Kwan Yew (msomi wa Chuo Kikuu cha Cambridge, Uingereza) – ambaye alitokana na ukoo wa ki-fisadi wa wacheza kamari – alitamka, “Singapore ilirithiwa bila ukanda wa bara; moyo bila mwili.”
Singapore iliamua kujijenga ili kujikomboa kutoka ma-dhambi, majuto na mavune ya miaka mingi kabla ya 1960. Ilipiga marufuku ma-kasino, kamari (iliyokuwa imefilisi ukoo wake), kuongeza kodi kwa tumbaku, na vinywaji vikali; na kudhibiti biashara ya madawa ya kulevya. Singapore ikawa ya walokoke.

Ili kudhibiti umaskini na mazoea yasiyo ya maadili mema, serikali ililivalia njuga suala la u-masikini. Singapore ilianza kufyeka na kujenga upya bandari na madhari yake, ingawa iliashiria kutambulika kama nchi itakayojiunga na maswaiba wa nchi fukara za Dunia ya Tatu. Lakini Singapore ilijinasua kuitwa hivyo!
Wafanyakazi walihimizwa kuchapakazi, mithili ya punda! Kwa mfano, siku moja ilimbidi huyo Waziri Mkuu Lee Kwan Yew akutane na Balozi wa Uingereza (akibeba ujumbe kutoka kwa Malkia wa Uingereza) akiwa hospitalini alikolazwa kutoka na uchovu na mavune ya kutolala kwa muda mrefu akichapakazi. Mkewe alikuwa ndiye daktari wake, na ilibidi kumpa dawa za usingizi au kumlaza (tranquilizers).

Singapore ilibadilika na kuwa kiota cha biashara, pesa na usafiri na kuwa jiji la kisasa (a prissy and trendy city). Ilijenga ma-kasino (mithili ya Las Vegas) na viota vya maraha, kwa mifano, Ministry of Sound ya London na Bangkong Q Bar, Velvet Underground, Vivo City Mall, jengo la zamani la watawa wa Convent of the Holy Infant Jesus sasa ni restauranti ya Chijmes, na hoteli za kuvutia, kama hiyo ya Fullerton Hotel (jengo la posta ya zamani) yenye kusifiwa huko Asia na kuna majumba ya ‘miendo ya paka’ kwa ajili ya ubunifu wa mavazi (fashion industry).
Zaidi, iliweka boti za fahari kwa watalii, madhahari safi, na mataa kila mahali ili kuvuta watalii kuzishinda Thailand na Malaysia na ilijenga majumba ya sinema, tamasha na burudani za utamaduni za wasanii wengi – waliokuwa wanapigwa marufuku mwanzoni na kukimbilia Bangkong, Thailand.

Viota vya minuso na maraha yake na burudani vilipigwa marufuku. Wasanii wengi walikimbilia Thailand na Malaysia. Ni hivi majuzi tu walipoaanza kuingiza hayo ya burudani na wafanyakazi kutakiwa kwa lazima kutabasamu ili kulegeza mavunde ya kazi!
Kulegeza u-Chapajikazi; Tabasamu
Wakati wa awamu ya pili, Singapore ilikuwa ni mojawapo ya nchi nne za Asia Mashariki kuitwa na Uingereza kwa jina la ‘Asian Tigers’. Zingine zilikuwa ni Hong Kong, Korea Kusini na Taiwan. Ma-bepari wa London mwaka 1995 (wakiongozwa na Waziri wa Fedha wa Uingereza Sir Kenneth Clarke na Makamu wa Rais wa Nchi za Ulaya Sir Leon Brittan) walipanga mkakati maalum wa kuhamasisha mfumo-kusudiwa kwa nchi hizo.

Mabepari hao mwaka 1996 walifanikiwa kumpata mweza wao Waziri Mkuu wa Singapore Goh Chok Tong (awamu ya pili) katika kuzindua mfumo-kusudiwa. Serikali ilifanikisha kuweka mipango kabambe ya elimu. Iliweka mikakati ya mustakabali wa taifa; ni wajibu wa serikali (sio wa sekta binafsi) kuandaa mipango ya elimu-kombozi ya taifa.
Wakati wa awamu ya pili chini ya Waziri Mkuu Goh Chok Tong mwaka 2004 na awamu ya sasa, chini ya Waziri Mkuu Lee Hsien Loong (mtoto wa Waziri Mkuu Lee Kwan Yew – shauri la siasa za kitanda kuzalisha viongozi wa nchi), serikali ilibidi kufungua madirisha (msemo wa ‘Mzee Ruksa’ mstaafu Rais Hassan Mwinyi) ili hewa ya maraha. Kuchapakazi kulilazimu kulegezwa (fine tuning) ikiwa ni pamoja na kuwataka wa-Singapore watabasamu ili kuficha uchovu na mavune ya kuchapakazi.

Zaidi, Serikali iljiingiza katika sakata la mipango na miradi ya maendeleo –sakata ambalo likiachiwa sekta binafsi, wachezaji watafanyiana rafu. Serikali ilikuwa na ubia na sekta binafsi na kuunda timu ya mipango na miradi ya maendeleo (ikiiga mfano wa Korea Kusini) na mabenki nchini yalishirikiana na wazalishaji huku ikipendelewa na Uingereza, Amerika na Benki Kuu ya Dunia ili icheze mchezo na ‘the big boys’.
Kama njiapanda ya kuingilia Asia Mashariki na ya Mbali kupitia Mlangobahari wa Malacca, Singapore ina vivutio vitatu muhimu: ‘location, location, location’, (a) kutoka na kuingilia Bahari ya Hindi; (b) kutoka na kuingilia Bahari ya China Kusini; na (c) uwanja wa ndege kwa sehemu hizo ikiwa ni pamoja na kuhudumia Bara la Australasia (Asia ya Mbali, Australia na New Zealand).

Leo hii, Singapore ni bandari-ghala (entrĂªport) kubwa kwa nchi zote za Australia, New Zealand na Asia Mashariki ya Mbali. Biashara ya huko ni kubwa sana; haiwezi kulinganishwa na biashara inayopita Dar es Salaam kwenda nchi za jirani!
Biashara nchini humo ilikuza miundombinu iliyojengwa kwa ajira ya unyonyaji wa mfumo wa manamba (wa-China, wa-Sri Lanka na wa-Hindi). Wananchi walitokana na mchanganyiko wa mataifa, dini na lugha nyingi, kwa mifano, wa-Uingereza, wa-Hindi, wa-Malalysia, wa-China na wa-Japani; dini nyingi, kwa mifano, wa-Budha, wa-Tao, wa-Islamu, wa-Confucius, wa-Kristo na wa-Hindu); na lugha nyingi, kwa mifano, ki-Ingereza, ki-Mandarini, ki-Malaysia, na ki-Tamili). Lakini leo hii kuna mataifa matatu makubwa” wa-Hindi, wa-China na wa-Malasia.

Waziri Mkuu awamu ya Tatu Lee Hsien Loong alipanua mianya ya biashara. Alitaka Singapore kutengeneza “fweza, fweza” kwa wingi. Aliruhusu watalii, na kuzidisha biashara kwa ajili ya kujenga tabaka la kati bila upendeleo.
Singapore ikatajirika kushinda nchi nyinginezo za Asia, ki-income per capita; Shirika la Ndege (Singapore Airlines) linaongoza duniani kwa sifa za juu; kiasi cha 90% ya wananchi wake wanaishi majumbani mwao; biashara inasheheni bila urasimu, ufisadi/rushwa na u-wazi (the freest).

Singapore inasifika kwa uwazi na utawala bora huku ikishindana kila mara kuwa ya kwanza; ilikataa kuwa namba mbili. Kuna majengo marefu na alama za utajiri. Mji ni msafi sana – hakuna uchafu wa mazingira. Bandari yake leo hii inag’aa kwa biashara.
Elimu ni ya kiwango cha juu na wengi wameelemika hadi chuo kikuu na wengi wamehitimu elimu-kazi/ajira kupitia vyuo vya ufundi (technicals and polytechnics) mbalimbali; wanatumia ‘internet’ ya spidi kali (broadband); kuna uhuru wa biashara na serikali inapendelea wawekezaji; kuna uwazi wa hali ya juu katika fani za kazi na biashara; na hakuna ufisadi na rushwa.

Kuna utawala bora; hakuna upendeleo kazini – wafanyakazi wanaajiriliwa na kupandishwa vyeo kulingana na sifa zao za ujuzi na ufanisi (meritocracy) – sio u-shemeji, u-kabila, u-dini, u-chumba, u-jomba, nk); wafanyakazi wa umma wanalipwa SAWA na wale wa sekta binafsi.
Serikali inaendeshwa kama bodi ya wakurugenzi wa kampuni/shirika binafsi; hakuna cha urasimu; na wala haikuachana na mfumo wa u-Koloni: elimu, lugha ya ki-Ingereza, mabarabara yalibakia na majina ya ki-Koloni.

Singapore ilipiga vita ubaguzi wa rangi na dini ili matunda ya uhuru yawafikie wananchi wote – maisha bora kwa kila m-Singapore! Mapato ya nchi yanagawanywa sawa miongoni mwa wananchi wenye asili tofauti: wa-Hindi, wa-China na wa-Malaysia; na inasemekana imetumia ufanisi wa kazi na hali halisi kwa ukatili zaidi kushinda serikali yeyote.
Kujenga Tabaka la Kati; Watengeneza/Wanunuzi ‘Goods/Services’ (Bidhaa na Huduma)

Singapore imetawaliwa mithili ya ki-dikiteta ikiongozwa na chama kimoja kikubwa na familia moja ya aliyekuwa Waziri Mkuu wa kwanza Lee Kwan Yew tangu uhuru! Singapore, yenye kutamba ‘maisha bora kwa wote’, imejengeka kwa ‘high-end’ za viwandani na mauzo kwa nchi za nje.
Kutokana na uhaba wa maliasili na ardhi ya kupanua, ilibidi ijikite katika kuzalisha huduma (high-end products or upmarket commodities) zilizolenga matajiri, kwa mfano, bidhaa fahari (magari, manukato, saa, kamera, komputa), majumba na mauzo ya vifaa vya uganga (biomedical exports) ambayo imesaidia sana nchi hiyo kufikia kukua kiasi cha 14% GDP (kutokana na mauzo ya biomedical exports).

Kama sikukosea, wastani wa ‘income per capita’ yake ni karibu $30,000; na ‘gross national product’ yake ni zaidi ya $182 bilioni. (Linganisha na Tanzania: i/c ni $440; GNP ni $20 bilioni).
Singapore imefanikiwa kuondoa tabaka la chini; tabaka wavuvi, makuli, malaya, wachuuzi wadogo, watembeza madaya ya kulevya na wengineo. Tabaka hili lilimezwa na wafanyakazi viwandani, maofisini na katika shughuli nyingine za huduma – tabaka la kati (middleclass) – lenye kuuza nguvu zake na kulipwa mishahara.

Hapo juu nimegusia suala la tabaka la wazalishaji. Mchambuzi mahiri wa mambo ya jamii m-Amerika Alvin Toffler analiita tabaka hili: ‘prosumers’; yaani, ‘producers and consumers’). Ninaliita, kwa kifupi, ‘wazalishalaji’ (wazalishaji na walaji).
Sisi hapa Tanzania, tabaka hili ni la wakulima, wafugaji, wawindaji au waokota porini, wahunzi/wasusi na machinga. Kwa ujumla, ni tabaka la wazalishaji na walaji wakati huo huo; yaani, tabaka la wenye kuzalisha na kuvitumia wazalishavyo (producers and consumers.

Kwa bahati mbaya, Tanzania imedhamiria kuliua tabaka hili la chini kwa kuandikisha ‘plots’ za mashamba na mfumo wa ufugaji huko vijijini ili utajiri (asset) huo utumike, kama rehani (collateral) ya kukopa mabenkini. Mabenki mengi sio ya wazawa; hivyo, mustakabali wa wazalishaji wetu utawekwa mikononi mwa wageni – wageni. Polepole, wageni wataanza kumiliki ardhi yetu!
Dhana za uchumi wa ki-Magharibi hauzingatii kabisa mchango wa wazalishaji! Nchi zinapimwa kwa kile kiitwacho, ‘income per capita’ (yaani, utajri wa mapesa kugawiwa sawa kwa wananchi) au ‘gross domestic national product’ (yaani, uzalishaji wote wa nchi ki-uchumi kwa mwaka).

Dhana hizo zinashindwa kubaini na kukubali kuwa vingi wa wazalishaji havipitii soko-pima! Kwa mfano, wazalishaji hawapati mahitaji yao kupitia ‘Shoprites’! Tunapimwa kwa mizani ya vigezo vya nchi ambazo ni ‘industrialized’ bila kujali kuwa Tanzania bado ni ‘prosumer’!
Chama Kimoja; Serikali Yaya-Mkali; Kufundisha Uungwana; Kudhibiti Tabia Mbaya
Singapore ni dola la yaya-mkali (a nanny State), chini ya chama-tawala kimoja chenye nguvu toka uhuru, People’s Action Party. Ilibidi serikali kujiuliza maswali (na kupata majibu) mazito kuhusu ni dunia ya namna gani Singapore inatakiwa kuishi ndani? Singapore inatoka, imefika, na inakwenda wapi? Je, ni vipi vya kufundisha mashuleni ili Singapore ifikie lengo lake?

Kuna malalamiko ya kuhujumu maisha ya mtu binafsi. Maslahi ya kundi ni juu ya yale ya u-binafsi kulingana itikadi ya ki-dini ya Confucianism na Uhuru wa binafsi haulindwi sana bali wa kundi. Hata hivyo, haifuati itikadi ya u-Jamaa au u-Komunisti.
Wananchi wanatii amri ya serikali/viongozi na kuheshimu wazee. Wazazi wanaweza kuwashitaki watoto wao kama wakikosa maadili. Dhana ya Confucianism ilijenga hulka ya utii au nidhamu ya woga na kudumaza ubunifu na uthubutu (creativity and risk-taking) kutokana na kuwa na viongozi waangalizi kila mahali.

Baadhi ya magazeti ya Ulaya yalipigwa marufuku kwa ubaguzi wa rangi (kwa mfano, gazeti la Cosmopolitan); hakukuwa na viota vya maraha na minuso; mabaa yalifungwa kabla walevi hawajavinjari kuweka nishai kidogo – watu ilikuwa ni kuchapajazi, kuchapakazi; na ukiangusha kishungi cha sigara, utafainiwa $328.
Ukichafua mazingira na majengo kwa graffiti au ukitema ‘chewing-gum’ barabarani, utachapwa viboko (ilinunuliwa kwa ruhusa ya daktari ili kulinda afya); ukipatikana na gramu 15 za heroin, utanyongwa kama unazidi miaka 18 (na imenyonga watu wengi); ukivuka taa za barabarani bila ruksa ya kwenda au kuendesha kuzidi spidi zilizoruhusiwa.

Kwenye majumba ya kupanga (yenye idadi ya wakazi 10%) usipovuta maji baada ya kutumia choo (kuna kamera za video) utatafutwa na polisi na kupewa adhabu; na kama hufuati maadili ya adabu kwenye kadamnasi, kwa mfano, kuongea kwa simu katika jumba la sinema au kutovuta maji msalani, utapelekwa kwenye taasisi za kurekebisha tabia (behaviour).
Zaidi, kama ukichelewa tafrija wakati wa arusi utapigwa faini na kama utawahi utatozwa $60 za vocha ya kununua chochote dukani; wanawake walihongwa wasizae, kama sungura; wenye akili walihimizwa kuoana; na wenye manywele marefu walipigwa marufuku.

Uhalifu nchini ni chini sana; kila kitu inakwenda kwa wakati (very efficient); hakuna foleni za magari kwenda au kutoka makazini kwa sababu ya ushuru wa kutumia barabara; na hakuna kuchafua mazingira na upandaji wa miti ulihimizwa kuufanya mji uwe wa kijanikibichi.
Singapore kujiingiza katika nyenzo muhimu za uchumi wake bila kuiachia sekta binafsi ili iweze kudhibiti mienendo ya uchumi. Inatoa ruzuku kwa wanafunzi waweze kufikia chuo kikuu (mfano wa Ujerumani) na kuruzuku makazi kwa kila mtu kuwa na nyumba kuliko kupanga.

Kuna vyuo mbalimbali vyenye kutoa elimu/ajira sio nadharia tu kwa kila mhitimu kuuzika na kupata ajira. Ina soko huru kabisa; hakuna cha ushuru wa vya kutoka nje. Mishahara ya chini, ajira pamoja na bima ya maisha kwa wananchi wote.
Zaidi, Singapore haifuati itikadi zilizoandikwa kwenye mbao za mawe za mkono wa kulia au kushoto – bora tu itikadi hiyo inaleta manufaa. Kila itikadi yenye manufaa kwa Singapore inapokelewa na kuahamishwa nchini (pragmatism); na inafuata na kuiga kutoka popote duniani (eclecticism), pia. Kwa kuchanganya u-bepari na u-jamaa (chini ya ‘yaya-mkali’), imeweza kuleta mafanikio kutoka ‘both worlds’.

Singapore ilifuata siasa ya kujitegemea (self-reliance and import substitutions policy). Wananchi walijimyima kununua vya anasa kutoka nje; sawa na kijito kunywesha mto, kunywesha bahari.
Ilijiwekea akiba kwa kwa upande wa wananchi na serikali na kuwawezesha wananchi wake kutofuja utajiri wao, serikali ilihimiza kutunza zaidi ya 20% ya GNP. Ni kutokana na sera hii Singapore ilifanikiwa kutunza karibu 42% ya GNP. Wananchi walihimizwa kununua vya nyumbani kuliko kununua vya kutoka nje.

Biashara kubwa ya huko Asia Mashariki ya Mbali ilikuwa ya haramu (the illegal ‘black” economy) yenye faida kubwa: u-malaya, madawa ya kulevya, riba ya uajiri (labor export brokerage fees), magendo ya silaha, wizi wa mafuta, kamari, ma-kasino, bahati nasibu za njia za panya na kupiga kamari mipirani.
Msomaji, umevisoma baadhi ya vigezo au viungo vya mapishi ya kuzikwamua nchi za Indonesia, Malaysia na Singapore. Umesoma, pia, namna Singapore ilivyojikwamua. Sijui umejifunza yepi ya kulinganisha na Tanzania yetu?

Kama nilivoandika hapo mwanzoni, pengine, cha maana kwetu sisi sio kurudufisha mifano ya Indonesia, Malaysia na Singapore kwa Tanzania. Hata hivyo, tunaweza kujifunza baadhi ya vigezo vichache na “very eclectically” na ‘pragmatically’ na kubakia na vilivyo ‘constructive’ kwa mustakabali wa Tanzania
Msomaji, makala yeyote haina budi kufikia mwisho.
Asante kwa kunisoma kwa kirefu na karibu kwa michango, nyongeza na maoni zaidi!

Naomba kuwasilisha.

Wednesday, May 23, 2012

Kizazi kipya na wasomi wapya

29 Feb 2012
Mwanafunzi Elifuraha John
jogofefu@yahoo.com
SAUT Tabora
Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine (SAUT)
+255-0769023574
Ndugu Mhariri,
ELIMU ni nyenzo muhimu katika kumkomboa mwanadamu katika nyanja zote za kimaisha. Elimu si tu kuingia darasani na kusoma vitabu bali ni kuwa na upeo mpana wa kuchanganua mambo yanayotokea katika jamii. Elimu makini na sahihi ni lazima imfanye mhitimu kuenzi tamaduni nzuri zilizopo katika jamii inayomzunguka. Msomi ni mtu anayepaswa kuigwa kwa matendo yake yenye hekima katika jamii.
Katika nchi yetu wasomi wengi “hawajisomi” na baadhi yao wamekuwa wakiishi mithili ya wanyama kwa kutotumia elimu yao katika kudadisi mambo. Ni watu wasiofuata na kuheshimu utamaduni wa kitanzania badala yake, wanasujudia utamaduni wa kigeni usiokuwa na manufaa kwa wanajamii. Mimi niko chuo kikuu nina ushahidi na haya ninayoeleza.
Kitambo nilifikiri kwamba elimu ingekuwa silaha nzuri sana kwa Mtanzania kujikomboa kifikra za kiutamaduni, lakini wapi. Elimu ndio imekuwa chombo cha kumfanya msomi kutojitambua kabisa. Leo hii wasomi wengi hasa wa vyuo vikuu baada ya kupata elimu, sasa wamepata nafasi ya kutembea nusu uchi kwa madaha.
Wamepata nafasi ya kuchubua ngozi kwa mikorogo mikali ili kufanana na mzungu, wamepata nafasi ya kuzungumza kwa kubana sauti kama manawali wa Ubelgiji na kuishi kwa utamaduni wa nchi za magharibi. Huyu ndiye msomi wetu wa leo hajitambui, hajithamini na wala hajielewi. Si wote wako hivyo la hasha! Wapo wengine wanaotambua umuhimu wao katika jamii na kujiheshimu kama wasomi.
Niliwahi kuandika makala mbili katika moja ya magazeti nchini Desemba, mwaka 2010, chini ya kichwa cha habari “hawa ndio wasomi wetu wa leo” na “kama huu ni uongo ukweli ni upi” nikijaribu kueleza hisia zangu juu ya mmomonyoko mkubwa wa maadili miongoni mwa wanazuoni wetu, baada ya kupata nafasi ya kujiunga na chuo kikuu.
Katika hali isiyotarajiwa, baadhi ya wanachuo waliopata kusoma makala zile walinishambulia kwa matusi na kunikejeli kwa madai ya kupotosha umma na kujenga mitazamo hasi dhidi ya wasomi wetu. Nilifikiri kuwa nimekosea lakini leo hii nimejiridhisha kwa uchunguzi niliofanya na kukiri kuwa wengi wa wasomi wetu ni chachu ya mmomonyoko wa maadili katika jamii zetu.
Mbali na hapo wengi wao ni wavivu wa kufikiri. Ni wasomi ambao wanapenda kusoma habari nyepesi katika magazeti ya udaku badala ya kutafuta habari muhimu ambazo ni za uhakika. Ni wavivu wa kusoma majarida na vitabu lakini badala yake wamewekeza bidii katika kusikiliza muziki hata kama hakuna ujumbe wa msingi kwao.
Sikatazi kusikiliza muziki bali tujitahidi kupembua na kudadisi mambo ya msingi. Hata mimi napenda kusikiliza muziki pale ninapochoka lakini wengi hatuko hivyo. Waangalie vijana wanaosoma katika taasisi mbalimbali za elimu wengi wao wanawaza kujilimbikizia mali pindi wanapopata nafasi nyeti za kazi au utawala waanze kula mpaka waote vitambi.
Wanawaza kuwa wezi wa mali ya umma na kuwa mafisadi hata kabla hawajapata fursa hizo maridhawa. Sasa wakipata itakuwaje? Kwa nchi kama hii yenye wananchi masikini, kama kila msomi atawaza kujilimbikizia mali kamwe hatutafikia maendeleo. Uzalendo kwa baadhi ya wanazuoni umetoweka kabisa. Maendeleo dhaifu katika nchi yetu ni matokeo ya Watanzania hasa wasomi kutanguliza maslahi yao binafsi kuliko ya jamii kwa ujumla.
Wasomi wengi wamekuwa bingwa wa kushabikia starehe hasa wale wa vyuo vikuu. Ukiyaeleza haya utaonekana adui wa umma. Lakini wale wenye utashi na walio makini watakubali ukweli huu usiopingika. Ndugu mhariri,naomba ieleweke kuwa barua hii haijumlishi wanazuoni wote bali ni wale wenye tabia niliyotaja hapo juu.
Kwa kuhitimisha, nafikiri kuna umuhimu wa kutilia mkazo suala la utamaduni na maadili bora katika ngazi zote za elimu ili kujenga jamii bora yenye maadili na inayowajibika. Hii ni pamoja na kuanzisha somo la maadili ya jamii katika mitaala yetu ya elimu.

Prof. Mwandosya: Afya kwanza urais baadaye

Tuesday, 22 May 2012 20:12
Rais Jakaya Kikwete akimsaidia kuteremka ngazi za Ikulu Prof Mark Mwandosya baada ya kumwapisha kuwa Waziri asiye na Wizara Maalumu, katika hafla iliyofanyika Ikulu jijini Dar es Salaam jana. Picha na Emmanuel Herman
Mwandishi Wetu
WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalumu), Profesa Mark Mwandosya, jana aliapishwa Ikulu kushika wadhifa huo huku akikataa kuzungumzia mipango yake ya baadaye ya kisiasa. Profesa Mwandosya akijibu moja ya maswali ya waandishi wa habari baada ya kuapishwa, lililohusu iwapo bado ana nia ya kugombea urais katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015, alisema hawezi kuzungumzia suala hilo mpaka hapo afya yake itakapotengemaa.

“Mbona mnapenda sana kuniuliza suala hili? Maana kila mwandishi akiniona anapenda kuuliza hili au leo mmeuliza kwa sababu mmeona nimekuja karibu na jengo hili? (Ikulu)…” alihoji huku akicheka na kuongeza: “Ngoja kwanza tuangalie afya…. Eeh! Afya kwanza halafu hayo mambo mengine yatafuata.” Profesa Mwandosya alihamishiwa Ofisi ya Rais kutoka Wizara ya Maji aliyokuwa akiiongoza awali, baada ya mabadiliko ya Baraza la Mawaziri yaliyofanywa na Rais Jakaya Kikwete, Mei 4, mwaka huu.

Hata hivyo, waziri huyo ambaye aliomba kugombea urais kupitia CCM akipamba na Rais Kikwete mwaka 2005, hakuweza kuapishwa na mawaziri wenzake Mei 7, mwaka huu kwa kuwa ndiyo kwanza alikuwa amerejea kutoka India alikokuwa kwa muda mrefu akipatiwa matibabu kutokana na ugonjwa ambao hata hivyo, haujawahi kuwekwa hadharani.

Katika mchakato wa kinyang’anyiro hicho ndani ya CCM, Profesa Mwandosya alishika nafasi ya tatu, nyuma ya Rais Kikwete na Dk Salim Ahmed Salim. Jana, Profesa Mwandosya alizungumzia afya yake kwa kusema kuwa anaendelea vizuri... “Afya yangu ni kama mnavyoiona, naendelea vizuri tu, mwaka jana nilikuwa nikitembea kwa msaada wa magongo lakini leo nimeweza kutembea mwenyewe bila msaada wa magongo, kwa kweli naendelea vizuri,” alisema Waziri huyo.

Kuhusu wadhifa wake mpya alisema anafahamu kwamba kazi aliyonayo ni kubwa na kwamba yuko tayari kumsaidia Rais katika majukumu mbalimbali ya kitaifa yanayomkabili. “Mnafahamu Rais ana majukumu mengi sana ya kitaifa, yanamhitaji kwenda hapa na pale, kwa hiyo mimi kwanza nashukuru kwa kupewa wadhifa huu na niko tayari kumsaidia mheshimiwa Rais katika majukumu hayo,” alisema.
Ugonjwa wake Profesa Mwandosya alikwenda katika Hospitali ya Apolo, India kwa ajili ya matibabu Mei, mwaka jana ambako alikaa huko kwa miezi ipatayo sita kabla ya kurejea Novemba 29, 2011.

Desemba 3, 2011 zikiwa zimepita siku sita tangu aliporejea, alifanya mkutano na waandishi wa habari katika makao makuu ya Wizara ya Maji na kusema kwamba alikuwa bado ana kiu ya kuwatumikia wananchi. Katika mkutano huo, Profesa Mwandosya alikataa kuzungumzia suala la urais wa 2015 kwa maelezo kwamba yapo mambo mengi ya kufanya na kwamba haukuwa wakati mwafaka.

“Kama kuna watu wana fedha za kuwekeza katika kutafuta uongozi ni wao, lakini mimi bado nahitaji kuwahudumia wananchi kwa kutatua matatizo ya maji,” alisema na kuongeza:

“Bado kuna mambo mengi, vilivyopo kwenye ajenda za Wizara ya Maji sijavikamilisha. Kwa hiyo siwezi kuzungumzia masuala ya urais wakati bado nina majukumu mazito ya kuwahudumia wananchi.” Januari mwaka huu, Profesa Mwandosya alikwenda tena India kuendelea na matibabu kabla ya kurejea nchini siku chache zilizopita.

1. MKATABA WA MUUNGANO BAINA YA JAMHURI YA TANGANYIKA NA JAMHURI YA WATU WA ZANZIBAR


    Kwa kuwa Serikali ya Jamhuri ya Tanganyika na Jamhuri ya watu wa Zanzibar zinafahamu uhusiano wa muda mrefu watu wake na mshikamano na kukuza uhusiano huo na kuimarisha mshikamano na kukuza umoja wa watu wa Afrika, zimekutana na kutafakari Muungano wa Jamhuri ya Tanganyika na Jamhuri ya watu wa Zanzibar.

    Na kwa kuwa Serikali za Jamhuri ya Tanganyika na Jamhuri ya watu wa Zanzibar, zinapendelea ya kwamba Jamhuri hizi mbili ziungane kuwa Jamhuri moja huru moja kwa amasharti ya makubaliano yafuatayo:

    Kwa hiyo IMEKUBALIWA baina ya Serikali ya Jamhuri ya Tanganyika na ya Jamhuri ya watu wa Zanzibar kama ifuatavyo:-

    I) Jamhuri ya Tanganyika na Jamhuri ya watu wa Zanzibar zitaungana na kuwa Jamhuri huru moja.

    II) Katika kipindi cha kuanza kwa Muungano mpaka Baraza la Kutunga katiba lililotajwa katika ibara ya (vii) litakapokutana na kupitisha katiba ya Jamhuri ya Muungano (Kuanzia hapa kitaitwa kipindi cha mpito), Jamhuri ya Muungano itaongozwa kwa masharti ya ibara ya (iii) mpaka ya (vi).

    III) Katika kipindi cha mpito katiba ya Jamhuri ya Muungano itakuwa katiba ya Tanganyika iliyorekebishwa ili kuweka:

    a) Chombo tofauti cha kutunga sheria na Serikali kwa ajili ya Zanzibar kwa mujibu wa sheria zilizopo za Zanzibar na vitakuwa na mamlaka ya mwisho katika Zanzibar kwa mambo yote isipokuwa yale tu yaliyo chini ya bunge na Serikali ya Jamhuri ya Muungano

    b) Nafasi ya makamo wawili wa Rais mmoja kati yao akiwa ni mkaazi wa Zanzibar atakuwa ndiye kiongozi wa Serikali iliyotajwa kwa ajili ya Zanzibar na atakuwa ndiye msaidizi mkuu wa rais wa Jamhuri ya Muungano katika utekelezaji wa kazi za Serikali kwa upande wa Zanzibar.

    c) Uwakilishi wa Zanzibar katika bunge la Jamhuri ya Muungano.

    d) Mambo mengine yatayofaa au kuhitajika ili kuipa nguvu Jamhuri ya Muungano na mkataba huu.

    IV) Mambo yafuatayo yatakuwa chini ya bunge na Serikali ya Jamhuri ya Muungano:-

    a) Katiba na Serikali ya Jamhuri ya Muungano
    b) Mambo ya nchi za nje
    c) Ulinzi
    d) Polisi
    e) Mamlaka yanayohusika na hali ya hatari
    f) Uraia
    g) Uhamiaji
    h) Mikopo na biashara ya nchi za nje
    i) Utumishi katika Jamhuri ya Muungano.
    j) Kodi ya mapato inayolipwa na watu binafsi na mashirika, ushuru wa forodha na ushuru wa bidhaa zinazotengenezwa nchini na kusimamiwa na idara ya forodha
    k) Bandari, mambo yanayohusu usafiri wa anga, Posta na Simu

    V) Bunge na Serikali vilivyotajwa vitakuwa na mamlaka ya mwisho juu ya mambo yote yahusuyo Jamhuri ya Muungano na kuongezea mamlaka juu ya mambo yote yahusuyo Tanganyika.

    Sheria zote zilizopo za Tanganyika na za Zanzibar zitaendelea kutumika katika maeneo yao bila kuathiri:-

    a) Masharti yoyote yatakayowekwa na chombo chenye mamlaka ya kutunga sheria.

    b) Masharti yatakayowekwa kwa amri ya Rais wa Zanzibar juu ya sheria yoyote inayohusu jambo lolote lililotajwa kwenye ibara ya (iv), na kufuta sheria yoyote inayolingana Zanzibar.

    c) Mabadiliko yoyote kama yataonekana yanafaa au kuhitajika ili kufanikisha Muungano na mkataba huu.

    a) Rais wa kwanza wa Jamhuri ya Muungano atakuwa ni Mwalimu J. K. Nyerere na ataongoza Serikali ya Jamhuri ya Muungano kwa kufuata masharti ya mkataba hu na kwa kusaidiwa na maofisa wengine atakaowateuwa toka Tanganyika na Zanzibar na watumishi wa Serikali zao.

    b) Makamo wa kwanza wa Rais kutoka Zanzibar aliyeteuliwa kwa kufuata marekebisho kama yalivyoelezwa na ibara ya 3, atakuwa Sheikh Abeid Karume.

    VI) Rais wa Jamhuri ya Muungano kwa kukubaliana na Makamo wa Rais ambaye ni kiongozi wa serikali ya Zanzibar

    a) Atateua tume kwa ajili ya kutoa mapendekezo kwa ajili ya katiba ya Jamhuri ya Muungano.
    b) Ataitisha Baraza la kutunga katiba ikiwa na wawakilishi kutoka Tanganyika na Zanzibar katika idadi itakayoamuliwa likutane katika kipindi cha mwaka mmoja tokea kuanza kwa muungano kwa madhumuni ya kutafakarimapendekezo ya tume iliyotajwa juu na kupitisha katiba ya Jamhuri ya Muungano.

    VII) Mkataba huu utahitaji kuthibitishwa kwa kutungiwa sheria na Bunge la Tanganyika na Baraza la Mapinduzi la Jamhuri ya Watu wa Zanzibar kwa kushirikiana na Baraza lake la Mawaziri, na mkataba kupitishwa na kuundwa kwa serikali ya Jamhuri ya Muungano na ya Zanzibar kwa kufuata masharti yaliyokubaliwa.

    KWA KUSHUHUDIA HAPA Julius K. Nyerere, Rais wa Jamhuri ya Tanganyika na abeid Karume, Rais wa Jamhuri ya Watu wa Zanzibar, wametia saini nakala mbili za mkataba huu, hapa Zanzibar siku ya tarehe Ishirini na mbili ya mwezi Aprili, 1964.

    ……………………………………………………………………………… …………………….
    Umepitishwa na Bunge siku ya tarehe Ishirini na Tano ya Aprili, 1964.


    ……………………………………………………………………………… …………………….
    Pius Msekwa, Karani wa Bunge

    ……………………………………………………………………………… …………………….
    Adam Sapi Mkwawa, Spika
    25 Aprili 1964

    xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx
    SOURCE:

    1: {THE PATNERSHIP, ISBN: 9789987880553, pg. 156, Author: Aboud Jumbe, }

    2: {Zanzibar hadi mwaka 2000: ISBN: 9789987898015, pg. 201, Author: Ali Shaaban Juma}
    xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx xxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxxx

1. HOTUBA YA MHESHIMIWA MIZENGO P. PINDA (MB)


1.     HOTUBA YA MHESHIMIWA MIZENGO P. PINDA (MB), WAZIRI MKUU WA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA WAKATI WA KUAHIRISHA MKUTANO WA SABA WA BUNGE LA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA – DODOMA, TAREHE 23 APRILI 2012

UTANGULIZI

Mheshimiwa Spika,
1. Nitumie nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa Rehema kwa kutuwezesha kutekeleza majukumu yote yaliyopangwa kwa ufanisi mkubwa katika Mkutano huu wa Saba wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ulioanza tarehe 10 Aprili 2012. Tumefanikiwa kufanya hivyo kutokana na maandalizi mazuri ya Mkutano, ushirikiano miongoni Mwetu na Waheshimiwa Wabunge wote kujiandaa vizuri katika kuchangia hoja mbalimbali zilizopangwa.

Mheshimiwa Spika,
2. Katika Mkutano huu, tumepata Waheshimiwa Wabunge Wapya Wawili wote kutoka Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA). Napenda kutumia nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Joshua Samwel Nassari kwa kuchaguliwa kuwa Mbunge Mpya wa Jimbo la Arumeru Mashariki. Vilevile, nampongeza Mheshimiwa Cecilia Daniel Paressokwa kuteuliwa kuwa Mbunge kupitia Viti Maalum (CHADEMA). Kipekee kabisa nawapongeza Wananchi wa Arumeru Mashariki kwa kutumia haki yao ya Kidemokrasia vizuri. Lakini kwa dhati kabisa, nakipongeza Chama Cha Mapinduzi kwa kukubali Matokeo ya Uchaguzi Mdogo wa Arumeru Mashariki. Kitendo hicho kinaonesha uungwana na ukomavu wa Kisiasa na Demokrasia katika Nchi yetu. Huu ni mfano mzuri wa kuigwa na Vyama vingine vyote vya Siasa Nchini.

3. Kwa Waheshimiwa Wabunge wapya tunawatakia mafanikio na tunawaahidi ushirikiano wetu ndani ya Bunge na katika Kujenga Taifa letu. Vilevile, napenda kutumia nafasi hii pia kuwapongeza Waheshimiwa Madiwani wote waliopata Ushindi katika Chaguzi zilizofanyika katika Kata za Vijibweni (Temeke), Kiwangwa (Bagamoyo), Kirumba (Mwanza), Logangabilili (Bariadi), Chang’ombe (Dodoma), Kiwira (Rungwe), Lizaboni (Songea) na Msambweni (Tanga). Tunawatakia wote waliochaguliwa afya njema na maisha mazuri ili muweze kuwatumikia Wananchi waliowachagua na Taifa kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika,
4. Katika Mkutano huu wa Saba wa Bunge tulifanya Uchaguzi wa Wawakilishi wa Nchi yetu katika Bunge la Jumuiya ya Afrika Mashariki. Napenda nitumie nafasi hii kuwapongeza wafuatao kwa kuchaguliwa kuwa Wabunge wa Bunge hilo, Mheshimiwa Makongoro Nyerere; Mheshimiwa Abdullah Hassan Mwinyi; Mheshimiwa Nderakindo Kessy; Mheshimiwa Angela Kizigha; Mheshimiwa Adam Kimbisa; Mheshimiwa Twaha Issa Taslima; Mheshimiwa Bernard Murunya; Mheshimiwa Shy-Rose Bhanji; na Mheshimiwa Mariam Ussi Yahya. Tunawapongeza Wote! Tuna imani kubwa kwamba watatuwakilisha vyema katika Bunge la Jumuiya ya Afrika ya Mashariki kwa maslahi ya Tanzania Kiuchumi na Kijamii na Nchi zote kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika,
5. Tangu kuhitimishwa kwa Mkutano wa Sita wa Bunge lako Tukufu, kumekuwepo na matukio mbalimbali ya kusikitisha, kusononesha, kuhuzunisha na yenye Majonzi makubwa yaliyosababishwa na Misiba na Ajali ambazo zimesababisha Vifo na kujeruhi Watanzania wenzetu wakiwemo Waheshimiwa Wabunge.

6. Napenda kupitia Bunge lako Tukufu, kutoa Salaam za Rambirambi kwa Familia, Ndugu, Jamaa na Marafiki wa Watanzania wote waliopoteza Maisha. Tuwaombee Marehemu wote ili Mwenyezi Mungu azilaze Roho zao Mahali Pema Peponi. Amina!

7. Vilevile, nawapa pole Majeruhi wote walionusurika na kupata Majeraha kutokana na Ajali mbalimbali zikiwemo ajali za Magari, Pikipiki, Baiskeli na vifaa vingine vya barabarani na ile ya Shirika la Ndege Nchini (ATCL) iliyotokea kule Kigoma.

Mheshimiwa Spika,
8. Wote tunafahamu kwamba katika kipindi hiki tumekuwa na Waheshimiwa Wabunge wenzetu ambao wamekuwa wakisumbuliwa na Maradhi mbalimbali. Tunamshukuru Mwenyezi Mungu kwa kusikia Maombi yetu. Wote tumefarijika kutokana na kurejea kwa Mheshimiwa Dkt. Harrison George Mwakyembe ndani ya Bunge lako Tukufu akiwa na Afya Njema. Tunaamini Afya yake itazidi kuimarika katika siku zijazo. Vilevile, ni matumaini yetu makubwa kwamba, wenzetu wengine akiwemo Mheshimiwa Profesa Mark James Mwandosya, Mbunge wa Jimbo la Rungwe Mashariki na Waziri wa Maji; Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, Mbunge wa Chato na Waziri wa Ujenzi; pamoja na Mheshimiwa Highness Samson Kiwia, Mbunge wa Ilemela ambao bado wako katika Matibabu watapata nafuu haraka itakayowawezesha kuungana na sisi tena ndani ya Bunge letu Tukufu.

Mheshimiwa Spika,
9. Mwisho, naungana na Watanzania wote kuipongeza Timu ya Simba kwa kufikia Mzunguko wa Tatu wa Mashindano ya Kombe la Mabingwa Barani Afrika. Sote tunawatakia Maandalizi mema ili wazidi kufanya vizuri katika Mechi zijazo kwa kuwa ushindi wao ni ushindi wa Nchi yetu. Kwa Wachezaji na Viongozi, wao nawaasa msibweteke na ushindi mlioupata, ila mnatakiwa kuelewa kuwa safari bado ni ngumu na ndefu.

SHUGHULI ZA SERIKALI

(a) Maswali

Mheshimiwa Spika,
10. Katika Mkutano huu wa Saba tunaouhitimisha leo, Jumla ya Maswali 131 ya Msingi na mengine 315ya Nyongeza kutoka kwa Waheshimiwa Wabunge yalipata majibu ya Serikali. Vilevile, jumla ya Maswali 16 ya Msingi na 9 ya Nyongeza kupitia utaratibu wa Maswali ya Papo kwa Papo kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu yalijibiwa.

(b) Miswada

Mheshimiwa Spika,
11. Katika Mkutano huu Miswada ifuatayo ilisomwa na kujadiliwa:
(i) Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali za Biashara wa Mwaka 2011 [The Business Laws (Miscellaneous Amendments) Bill, 2011];

(ii) Muswada wa Sheria ya Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania wa Mwaka 2011 (The Tanzania Livestock Research Institute Bill, 2011);

(iii) Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria za Mifuko ya Hifadhi ya Jamii wa Mwaka 2012 [The Social Security Laws (Amendments) Act, 2012]; na

(iv) Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali wa Mwaka 2011 [The Written Laws (Miscellaneous Amendments) (No.2) Act, 2011].
Vilevile, Muswada wa Sheria ya Haki za Wagunduzi wa Mbegu za Mimea wa Mwaka 2012 [The Plant Breeder’s Rights Bill, 2012] ulisomwa kwa mara ya kwanza.

(c) Taarifa Mbalimbali

Mheshimiwa Spika,
12. Bunge lako Tukufu lilipata fursa ya kupokea na kujadili Taarifa mbalimbali kama ifuatavyo:

(i) Taarifa za Kamati za Bunge zinazosimamia Fedha za Umma; na

(ii) Taarifa za Kamati za Bunge za Kisekta na zisizo za Kisekta.


Mheshimiwa Spika,
13. Napenda nitumie nafasi hii kuwashukuru kwa dhati Waheshimiwa Wabunge wote kwa kazi nzuri ambayo wameifanya katika siku zote za Mkutano huu zikiwemo kujadili na kupitisha Miswada niliyotaja hapo juu. Nawashukuru pia kwa michango yenu wakati wa kujadili Taarifa mbalimbali zilizowasilishwa hapa Bungeni.

Mheshimiwa Spika,
14. Kipekee kabisa nitumie nafasi hii kuwapongeza Wenyeviti na Wajumbe wa Kamati za Bunge zilizowasilisha Taarifa mbalimbali mbele ya Bunge lako Tukufu. Ni dhahiri kuwa utaratibu huu unatoa fursa kwa Waheshimiwa Wabunge kupitia kwa kina masuala mbalimbali ya Kisekta na kutoa ushauri kwa Serikali. Aidha, utaratibu huu unatusaidia kuwepo kwa ‘Checks and Balances’ ndani ya Nchi yetu. Niwashukuru pia Wabunge wote kwa jinsi walivyochangia kwenye mjadala wa kujadili Taarifa hizo.

Waheshimiwa Wabunge wameonesha hisia zao katika kujadili masuala yote haya muhimu na mengineyo na hasa katika Mwenendo wa Matumizi ya Fedha za Serikali kwenye Wizara, Taasisi za Umma, Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa. Nawashukuru sana kwa kujadili Taarifa zote kwa uwazi na hatimaye kutoa mapendekezo kwa Serikali namna ya kushughulikia matatizo yaliyojitokeza kwenye maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Spika,
15. Mapendekezo ya Waheshimiwa Wabunge yako katika makundi muhimu yafuatayo:

Kwanza: Ni uimarishaji wa Uongozi na Utendaji katika Wizara, Taasisi za Serikali, Mashirika ya Umma, Mikoa na Serikali za Mitaa;

Pili: Ni usimamizi wa Sheria, Kanuni na Taratibu zinazohusu masuala ya Mapato na Matumizi ya Fedha;

Tatu: Ni uimarishaji wa hatua za Kupambana na Rushwa, Ubadhirifu na Wizi wa Mali za Umma;

Nne: Ni uendelezaji wa hatua za kubana matumizi yasiyo ya lazima ndani ya Serikali na Vyombo vyake; na

Tano: Ni ulinzi wa Rasilimali za Nchi kwa maslahi ya Taifa letu.

Mheshimiwa Spika,
16. Siku zote Serikali imekuwa tayari kupokea ushauri wa Bunge lako Tukufu na baada ya kusikiliza mjadala na mapendekezo ya Waheshimiwa Wabunge, Serikali inaahidi kufuatilia kwa karibu utekelezaji wa Ushauri na Mapendekezo yaliyomo katika Taarifa hizo. Niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba Serikali itachukua hatua stahiki kuimarisha usimamizi na utendaji ndani ya Wizara na Serikali za Mitaa na Vyombo vyake na kuhakikisha Viongozi na Watendaji wake wanafanya kazi kwa umakini na uadilifu zaidi.

Mheshimiwa Spika
17. Katika Hotuba yangu hii ningependa kuzungumzia kwa kifupi mambo machache yanayohusu: Hatua zilizofikiwa katika Mchakato wa Kutekeleza Sheria ya Mabadiliko ya Katiba; Dhana ya Mifuko ya Hifadhi ya Jamii; Matokeo ya Shule za Msingi na Kidato cha Nne Mwaka 2011; Maendeleo ya Viwanda; Sensa ya Watu na Makazi; na mwisho Mpango wa Kutoa Kifuta Machozi cha Mifugo.

HATUA ZILIZOFIKIWA KATIKA MCHAKATO WA KUTEKELEZA SHERIA YA MABADILIKO YA KATIBA

Mheshimiwa Spika,
18. Kama Waheshimiwa Wabunge watakavyokumbuka, katika Mkutano wa Sita mwezi Februari 2012, Bunge lako Tukufu lilijadili na kupitisha Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba (Sura ya 83). Napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kuwa, mara baada ya Marekebisho hayo kupitishwa, Mheshimiwa Rais Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete kupitia Tangazo la Serikali Namba 66 la tarehe 24 Februari 2012; alialika Vyama vya Siasa vyenye Usajili wa Kudumu, Jumuiya za Dini, Asasi za Kiraia, Taasisi na Makundi ya Watu wenye malengo yanayofanana kuwasilisha kwake majina ya watu wanaoweza kuteuliwa kuwa Wajumbe wa Tume itakayoratibu na kukusanya maoni ya Wananchi kuhusu Mabadiliko ya Katiba.

19. Kwa mujibu wa Tangazo hilo, siku ya mwisho ya kuwasilisha mapendekezo ya majina ilikuwa tarehe 16 Machi 2012. Hata hivyo, kutokana na umuhimu wa zoezi hilo na ili kutoa fursa zaidi kwa Wananchi na Taasisi au Makundi yaliyopo Mikoani, Mheshimiwa Rais kupitia Tangazo la Serikali Namba 101 la tarehe 16 Machi 2012 aliongeza muda huo hadi tarehe 23 Machi 2012. Mapendekezo ya majina yaliyopokelewa yalikuwa mengi na hivyo kumpa Mheshimiwa Rais uwanja mpana zaidi wa kufanya uteuzi.

Mheshimiwa Spika,
20. Tarehe 6 Aprili 2012, Mheshimiwa Rais baada ya kushauriana na Mheshimiwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, aliteua Wajumbe 32 wa Tume itakayoratibu na Kukusanya Maoni ya Wananchi kuhusu Mabadiliko ya Katiba. Pamoja na Wajumbe hao, Mheshimiwa Rais aliteua Katibu na Naibu Katibu wa Tume hiyo. Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti, Wajumbe, Katibu na Naibu Katibu wa Tume waliapishwa na Mheshimiwa Rais tarehe 13 Aprili 2012. Kutokana na umuhimu wa Tume hii katika historia ya Nchi yetu, naomba niwataje Wajumbe wote wa Tume walioteuliwa:
1. Mheshimiwa Jaji Joseph Sinde WARIOBA – Mwenyekiti;
2. Mheshimiwa Jaji Mkuu Mstaafu, Augustino RAMADHANI -Makamu Mwenyekiti;
3. Mheshimiwa Dkt. Salim Ahmed SALIM – Mjumbe;
4. Ndugu Abubakar Mohammed ALI – Mjumbe;
5. Ndugu Ally Abdullah Ally SALEH – Mjumbe;
6. Mheshimiwa Al-Shaymaa J. KWEGYIR (Mb.) – Mjumbe;
7. Ndugu Awadh Ali SAID – Mjumbe;
8. Dkt. Edmund Adrian Sengondo MVUNGI – Mjumbe;
9. Ndugu Esther P. MKWIZU – Mjumbe;
10. Ndugu Fatma Said ALI – Mjumbe;
11. Ndugu Humphrey POLEPOLE – Mjumbe;
12. Ndugu Jesca Sydney MKUCHU – Mjumbe;
13. Ndugu John J. NKOLO – Mjumbe;
14. Ndugu Joseph BUTIKU – Mjumbe;
15. Ndugu Kibibi Mwinyi HASSAN – Mjumbe;
16. Ndugu Maria Malingumu KASHONDA – Mjumbe;
17. Ndugu Muhammed Yussuf MSHAMBA – Mjumbe;
18. Ndugu Mwantumu Jasmine MALALE – Mjumbe;
19. Prof. Mwesiga L. BAREGU – Mjumbe;
20. Ndugu Nassor Khamis MOHAMMED – Mjumbe;
21. Ndugu Omar Sheha MUSSA – Mjumbe;
22. Prof. Palamagamba J. KABUDI – Mjumbe;
23. Mheshimiwa Raya Suleiman HAMAD – Mjumbe;
24. Ndugu Richard Shadrack LYIMO – Mjumbe;
25. Ndugu Riziki Shahari MNGWALI – Mjumbe;
26. Alhaj Said EL- MAAMRY – Mjumbe;
27. Ndugu Salama Kombo AHMED – Mjumbe;
28. Ndugu Salma MAOULIDI – Mjumbe;
29. Ndugu Simai Mohamed SAID – Mjumbe;
30. Ndugu Suleiman Omar ALI – Mjumbe;
31. Ndugu Ussi Khamis HAJI – Mjumbe;
32. Ndugu Yahya MSULWA – Mjumbe;
33. Ndugu Assaa Ahmad RASHID – Katibu; na
34. Ndugu Casmir Sumba KYUKI – Naibu Katibu.

Mheshimiwa Spika,
21. Kwa namna ya pekee, nampongeza Mheshimiwa Jaji Joseph Sinde Warioba, Waziri Mkuu na Makamu wa Kwanza wa Rais Mstaafu kwa kuteuliwa kuwa Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba na Mheshimiwa Augustino Ramadhani, Jaji Mkuu Mstaafu wa Tanzania kwa kuteuliwa kuwa Makamu Mwenyekiti. Vilevile, napenda kuwapongeza Wajumbe wote, wakiwemo Katibu na Naibu Katibu kwa kuteuliwa kuunda Tume hii. Ni matumaini yangu na ya Watanzania wote kwa ujumla kuwa, Wajumbe wa Tume watatumia ujuzi, maarifa na uzoefu wao katika kuhakikisha wanatekeleza majukumu waliyopewa kwa mujibu wa Sheria na kwa ufanisi mkubwa.

Serikali ilivyojipanga (Maandalizi ya Tume)

Mheshimiwa Spika,
22. Wakati wa hafla ya kuwaapisha Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti, Wajumbe, Katibu na Naibu Katibu wa Tume, Mheshimiwa Rais aliihakikishia Tume kuwa Serikali itaipa kila aina ya ushirikiano ili itekeleze majukumu yake kwa ufanisi. Kwa niaba ya Serikali kupitia Bunge lako Tukufu, naomba kwa mara nyingine tena nikuhakikishie kuwa Serikali imejipanga kwa kuweka mazingira yatakayoiwezesha Tume kutekeleza majukumu yake kama Sheria ya Mabadiliko ya Katiba (Sura ya 83) inavyoelekeza. Hivi sasa, Serikali inakamilisha maandalizi muhimu kuiwezesha Tume kuanza kazi tarehe 1 Mei 2012 kama ilivyopangwa.

Mheshimiwa Spika,
23. Naomba kutumia fursa hii kuwaomba Wananchi wote kuipa Tume ushirikiano wa kutosha ili iweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi. Vilevile, napenda kuwasihi Wananchi wajitokeze kwa wingi katika Mikutano itakayoitishwa na Tume na watoe maoni yao kwa uhuru na utulivu bila vikwazo vyovyote. Lengo la Serikali ni kuhakikisha kuwa Watanzania wote wanashiriki kikamilifu bila ubaguzi wowote katika mchakato huo wa kuandika Katiba Mpya ili Nchi yetu iweze kupata Katiba itakayokidhi mahitaji ya Karne hii na miaka mingi ijayo.

Mheshimiwa Spika,
24. Napenda kusisitiza maagizo ya Mheshimiwa Rais aliyoyatoa siku ya kuwaapisha Wajumbe wa Tume kwamba Mchakato huu wa Mabadiliko ya Katiba siyo mchakato wa kuwepo au kutokuwepo kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Huu ni mchakato unaolenga kukubaliana namna bora ya kuendesha Nchi kwa kuzingatia uwepo wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, uwepo wa Haki za Binadamu na Misingi ya Utawala Bora, uwepo wa Mihimili Mitatu ya Dola yaani Bunge, Mahakama na Serikali na namna nzuri ya kuboresha utendaji kazi wa Mihimili hiyo. Ninawaomba Waheshimiwa Wabunge kuwaelimisha Wananchi juu ya kuzingatia mambo haya ya msingi wakati wa kutoa maoni yao.
MIFUKO YA HIFADHI YA JAMII

Mheshimiwa Spika,
25. Waheshimiwa Wabunge watakumbuka kuwa Bunge lako Tukufu lilipitisha Sheria Namba 8 ya Mwaka 2008 ya kuanzisha Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii.Umuhimu wa Hifadhi ya Jamii Nchini unatambuliwa ndani ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Ibara ya 11(1) inayosomeka, nanukuu:

“Mamlaka ya Nchi itaweka utaratibu unaofaa kwa ajili ya kufanikisha utekelezaji wa Haki ya Mtu Kufanya Kazi, Haki ya kujipatia Elimu na Haki ya kupata Msaada kutoka kwa Jamii wakati wa Uzee, Maradhi au hali ya Ulemavu, na katika hali nyinginezo za mtu kuwa hajiwezi.” Mwisho wa kunukuu.

Hivyo, Hifadhi ya Jamii ni nguzo muhimu katika kutekeleza dhana ya Utawala Bora katika Jamii na kuchochea ukuaji wa Uchumi.

Mheshimiwa Spika,
26. Lengo Kuu la kuwa na Mipango ya Hifadhi ya Jamii ni kuondoa Umaskini wakati wa Uzee na kutoa kinga ya Kiuchumi na Kijamii pale panapotokea matukio na majanga mbalimbali yanayosababisha kupungua kwa kipato. Hivi sasa kuna Mifuko Sita ya Hifadhi ya Jamii ambayo inatoa Mafao ya muda mfupi na muda mrefu kulingana na taratibu zilizopo katika Sheria za Mifuko husika. Mifuko hiyo ni Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF); Mfuko wa Pensheni kwa Mashirika ya Umma (PPF); Mfuko wa Pensheni kwa Watumishi wa Umma (PSPF); Mfuko wa Pensheni kwa Watumishi wa Serikali za Mitaa (LAPF); Mfuko wa Akiba kwa Watumishi wa Serikali (EGPF); na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF).

Mheshimiwa Spika,
27. Kwa mujibu wa takwimu zilizopo, ni Asilimia 5.9tu ya nguvu kazi ya Watanzania waliopo katika Sekta rasmi ndiyo wanaopata huduma ya Mifuko ya Hifadhi ya Jamii. Takwimu hizi ni kielelezo tosha kuonesha changamoto inayoikabili Sekta ya Hifadhi ya Jamii katika kuhakikisha Watanzania wengi wanajiunga na kunufaika na Mifuko ya Hifadhi ya Jamii. Aidha, changamoto hii si kwa Wananchi wanaojishughulisha katika Sekta isiyo rasmi tu bali hata kwa wale waliopo katika Sekta rasmi ambao kwa namna moja au nyingine hawajajiandikisha katika Mifuko ya Hifadhi ya Jamii.

Mheshimiwa Spika,
28. Changamoto nyingine zinazokabili Mifuko hii ya Hifadhi ya Jamii ni pamoja na kupishana sana kwa Mafao kati ya Mfuko mmoja na mwingine japo kiwango cha kuchangia kinalingana yaani Asilimia 20 ya Mshahara wa Mtumishi. Lipo pia tatizo la Pensheni isiyoendana na gharama za maisha, gharama kubwa za uendeshaji wa Mifuko, huduma hafifu kwa Wanachama wa Mifuko, Kukosekana kwa Kanuni za Uwekezaji zinazolingana pamoja na Idadi kubwa ya Wananchi kutoelewa umuhimu wa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii.

Mheshimiwa Spika,
29. Katika kukabiliana na baadhi ya changamoto zilizoko kwenye Sekta hii ya Hifadhi ya Jamii, Serikali imechukua hatua mbalimbali. Moja ya hatua hizo ni kuanzisha na kutekeleza Sera ya Taifa ya Hifadhi ya Jamii ya mwaka 2003 ambayo ni Dira ya shughuli zote za Hifadhi ya Jamii hapa Nchini. Vilevile, mwaka 2008 Serikali ilianzisha Mamlaka ya Hifadhi ya Jamii. Jukumu kubwa la Mamlaka hii ni kusimamia Sekta ya Hifadhi ya Jamii ikiwamo Mifuko yote ya Hifadhi ya Jamii Nchini. Ni matumaini yangu kuwa Mamlaka ya Hifadhi ya Jamii itatusaidia kuzifanyia kazi Changamoto nilizozitaja hapo juu na nyingine ili kuhakikisha kuwa Watanzania wengi wanajiunga na kupata Hifadhi ya Jamii.

Mheshimiwa Spika,
30. Ili kuhakikisha kuwa Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii, Serikali ilileta katika Kikao hiki cha Bunge Muswada wa Marekebisho ya Sheria za Mifuko ya Hifadhi ya Jamii. Nichukue fursa hii kulipongeza Bunge lako Tukufu kwa kupitisha Muswada huu. Muswada huo uliopitishwa na Bunge unalenga kuwianisha Sheria za Mifuko na Sheria ya Mamlaka ya Hifadhi ya Jamii. Lengo ni kuipa Mamlaka uwezo zaidi wa kutekeleza majukumu yake; na kuiwezesha Mifuko kutoa huduma bora kwa Wanachama wake. Muswada huu unaiwezesha pia Mifuko kutambua uwezo wa Mamlaka kuleta mageuzi kwenye Sekta kwa kutoa Miongozo mbalimbali.
Mheshimiwa Spika,
33. Nachukua fursa hii kuwakumbusha Waajiri wanaokiuka Sheria kwa kuwachagulia Wafanyakazi wao wapya, Mifuko ya kujiunga nayo kinyume na matakwa ya Wafanyakazi hao waache kufanya hivyo. Kila Mwajiri anatakiwa kuweka mazingira yatakayomwezesha Mfanyakazi kuchagua Mfuko anaoupenda. Mazingira hayo ni pamoja na kuialika Mifuko yote kutoa maelezo kuhusu Mafao na huduma zao na kuwapa fursa Wafanyakazi kufanya maamuzi ya kujiunga na Mfuko waupendao. Ni matumaini yangu kuwa Mamlaka itaweka Kanuni zitakazowezesha Mifuko kuandikisha Wanachama kwa utaratibu unaokubalika na unaomlinda Mwanachama.

34. Kwa upande wa Uwekezaji, Mamlaka imekamilisha tathmini ambayo itawezesha kutengeneza Miongozo kwa Mifuko kuwekeza katika Vitega Uchumi mbalimbali. Vilevile, Mamlaka itaweka mkakati kabambe wa kuelimisha Umma ili Wananchi wengi zaidi waweze kujiunga na Mifuko hii kwa kuwa sasa wanaruhusiwa kujiunga na Mifuko hiyo bila kujali kama wako Sekta Rasmi au isiyo Rasmi. Napenda pia kutumia fursa hii kutoa wito kwa Waheshimiwa Wabunge na Wananchi wote kutoa ushirikiano stahiki kwa Mamlaka ili kwa kushirikiana na Wadau mbalimbali tuboreshe, tuimarishe na kuwa na Sekta ya Hifadhi ya Jamii iliyo endelevu.

MATOKEO YA MTIHANI WA KUMALIZA ELIMU YA MSINGI MWAKA 2011

Mheshimiwa Spika,
35. Mwaka 2011 Wanafunzi 983,545 wa Darasa la Saba walifanya mtihani wa Taifa. Kati yao Wanafunzi 567,567,sawa na Asilimia 58.28 ya waliofanya mtihani walifaulu. Kiwango cha Ufaulu cha mwaka 2011, ikilinganishwa na kile cha mwaka 2010 unaonesha kupanda kwa Asilimia 4.76 kutoka Asilimia53.52 ya mwaka 2010 hadi 58.28 mwaka 2011.

Mheshimiwa Spika,
36. Tathmini inaonesha Ufaulu kimasomo umeongezeka kwa masomo ya Hisabati, Kiingereza na Sayansi.
i) Kiwango cha Ufaulu kwa Somo la Hisabati kilikuwa Asilimia 39.4 mwaka 2011ikilinganishwa na Asilimia 24.7 mwaka 2010;

ii) Kiwango cha Ufaulu kwa Somo la Kiingereza kilikuwa Asilimia 46.7 mwaka 2011ikilinganishwa na Asilimia 36.5 mwaka 2010; na

iii) Kiwango cha Ufaulu kwa Somo la Sayansi kilikuwa Asilimia 61.3 mwaka 2011 ikilinganishwa na Asilimia 56.1 mwaka 2010.

37. Taarifa zinaonesha kuwa kiwango cha ufaulu kwa masomo ya Kiswahili na Maarifa ya Jamii kilishuka kwa mwaka 2011 ikilinganishwa na mwaka 2010. Kwa mfano, Ufaulu kwa Somo la Kiswahili ulikuwa Asilimia 68.6 mwaka 2011 ikilinganishwa na Asilimia 71.0 mwaka 2010; na kiwango cha ufaulu kwa Somo la Maarifa ya Jamii kilikuwa Asilimia 54.8 mwaka 2011 ikilingnishwa na Asilimia 68.0 mwaka 2010.

Mheshimiwa Spika,
38. Ni kweli kwamba, kwa muda mrefu tumekuwa na matatizo ya ufaulu katika masomo ya Sayansi Nchini, lakini matokeo ya mwaka 2011 yanaonesha kuwa juhudi zinazochukuliwa na Serikali katika kukuza masomo hayo zimeanza kuzaa matunda. Napenda kuwapongeza Wanafunzi, Wazazi, Walezi, Walimu na Watendaji wote walioshiriki katika kuleta mafanikio hayo.

Uchaguzi wa Wanafunzi kuingia Kidato cha Kwanza mwaka 2012

Mheshimiwa Spika,
39. Katika Uchaguzi wa kuingia Kidato cha Kwanza mwaka 2012, jumla ya Wanafunzi 515,187, sawa na Asilimia 90.1 ya Wanafunzi waliofaulu walichaguliwa kuingia Kidato cha Kwanza katika Shule za Sekondari za Serikali. Idadi hii iliongezeka kwa Asilimia 12.49 kutoka Wanafunzi 456,350 mwaka 2010. Taarifa nilizopokea kutoka Mikoa 12 ya Arusha, Dar es Salaam, Dodoma, Iringa, Mara, Morogoro, Mwanza, Lindi, Kilimanjaro, Pwani, Ruvuma na Tanga,
zinaonesha kuwa Wanafunzi wote waliofaulu wamejiunga na Kidato cha Kwanza. Nitumie nafasi hii kuipongeza Mikoa hii kwa kuhakikisha kuwa hakuna Wanafuzi waliofaulu na kushindwa kujiunga na Sekondari.

40. Hata hivyo, sehemu kubwa ya Mikoa niliyoitaja inaonesha kuwepo kwa uhaba mkubwa wa Vyumba vya Madarasa na Madawati. Naiagiza Mikoa yote kuhakikisha mapungufu haya yanashughulikiwa katika Bajeti ya mwaka 2012/2013. Aidha, Mikoa iwe na Mipango endelevu ya kujenga Vyumba vya Madarasa na kutengeneza Madawati badala ya kusubiri matokeo ya Mtihani na kuchaguliwa kwa Wanafunzi ndipo ianze kuweka mikakati.

Matokeo ya Kidato cha Nne mwaka 2011

Mheshimiwa Spika,
41. Matokeo ya Kidato cha Nne ya mwaka 2011 yanaonesha kuwa Wanafunzi 181,880, sawa na Asilimia 53.6ya Wanafunzi 339,330 waliofanya Mtihani walifaulu. Kiwango hicho kimeongezeka kutoka Wanafunzi 177,011 waliofaulu mwaka 2010 ikiwa ni sawa na Asilimia 50.4 ya Wanafunzi 351,214 waliofanya Mtihani.

Mheshimiwa Spika,
42. Tangu mwaka 2008, Asilimia ya Wanafunzi wanaofeli Mitihani ya Kidato cha Nne imekuwa ikiongezeka na kufikia Asilimia 16.3,mwaka 2009 Asilimia 27.5, mwaka 2010 Asilimia 49.6 na kushuka tena hadi Asilimia 43.3, mwaka 2011. Sababu za kushuka kwa ufaulu huo ni pamoja na upungufu wa Walimu, Vifaa vya Kufundishia na kujifunzia na kuimarika kwa udhibiti wa uvujaji wa mitihani ya Kidato cha Nne. Vilevile, inaelezwa na Wanataaluma na Watafiti kwamba kuondolewa kwa Mtihani wa Kidato cha Pili kumechangia sana matokeo mabaya ya Kidato cha Nne.

Mheshimiwa Spika,
43. Kutokana na hali ya kuongezeka kwa idadi ya Wanafunzi wanaofeli Mtihani wa Kidato cha Nne, Serikali imechukua hatua kadhaa zikiwemo za kuongeza na kuimarisha usimamizi wa matumizi ya ‘capitation grant’ ili kupunguza tatizo la upungufu wa Vifaa vya Kufundishia na Kujifunzia Shuleni; Kutekeleza mikakati ya kuongeza idadi na ubora wa Walimu; na kujenga uwezo wa Wakuu wa Shule kusimamia ufundishaji na ujifunzaji wa kila siku.

44. Ni matarajio yangu kwamba tukiyafanya haya, tutaweza kufikia Azma yetu ya kuwa na matokeo mazuri katika siku zijazo. Niwaombe Wadau wote wa Elimu wakiwemo Waheshimiwa Wabunge, Viongozi, Walimu, Wazazi, Walezi na Wanafunzi kila mmoja atimize wajibu wake katika utoaji wa Elimu kuanzia, Nyumbani, Shuleni na Vyuoni ili tuweze kuinua Kiwango cha Ubora wa Elimu Nchini.

MAENDELEO YA VIWANDA

Mheshimiwa Spika,
45. Tarehe 16 hadi 23 Septemba 2011 nilifanya ziara Mkoa wa Mara na kutembelea Kiwanda cha Nguo cha Musoma Textile (MUTEX). Tarehe 2 hadi 4 Desemba 2011 nilifanya ziara nyingine fupi Mkoa wa Mwanza na kutembelea Kiwanda cha kutengeneza Nguo cha Mwanza Textile (MWATEX). Kwa kweli nilikuta Viwanda hivyo vinakabiliwa na changamoto nyingi zikiwemo za kukosekana kwa umeme wa uhakika, Wataalam na teknolojia ya kisasa. Nilielezwa kuwa changamoto hizo zinavikabili Viwanda vingi vya Nguo Nchini.

Mheshimiwa Spika,
46. Sote hapa tunafahamu kuwa maendeleo makubwa na ya kasi kwenye Nchi mbalimbali Ulimwenguni yalichangiwa kwa kiasi kikubwa na maendeleo ya Viwanda vya Nguo na Mavazi. Viwanda hivi hutoa Soko la uhakika kwa zao la Pamba linalolimwa hapa Nchini; huajiri kiasi kikubwa cha Wafanyakazi na hivyo kuwa na mchango mkubwa katika kupunguza tatizo la ajira na umaskini hasa miongoni mwa Vijana. Pia, huchangia Mapato kwa Serikali na Mifuko ya Hifadhi ya Jamii. Kutofanya vizuri kwa Viwanda hivi kunaikosesha Serikali na Wananchi Mapato na kuongeza tatizo la ajira Nchini. Niliona kuna umuhimu wa kutafuta ufumbuzi wa changamoto zilizo ndani ya uwezo wa Serikali.

Mheshimiwa Spika,
47. Tarehe 23 Machi 2012, niliitisha Mkutano wa Wadau wa Sekta Ndogo ya Viwanda vya Mavazi na Nguo ili kwa pamoja tuweze kuainisha changamoto zinazoikabili Sekta hiyo na kupata mapendekezo ya namna ya kukabiliana na changamoto hizo. Kufuatia Mkutano huo, iliundwa Timu ya Wataalam ili iweze kuangalia changamoto hizo kwa kina na kutoa mapendekezo ya hatua za kuchukuliwa na Serikali pamoja na Wadau wote ili kukabiliana na changamoto hizo. Timu hiyo ilipewa mwezi mmoja na wakati wowote kuanzia sasa itawasilisha taarifa yake Serikalini.

Mheshimiwa Spika,
48. Tarehe 15 Aprili 2012, nilipata fursa ya kutembelea viwanda vya Sunflag (Tanzania) Ltd, Kiwanda cha A to Z na Minjingu Mines and Fertilizer Limited vyote vya Mkoani Arusha. Katika Viwanda vya Nguo vya Sunflagna A to Z nilifarijika kuona idadi kubwa ya Watumishi walioajiriwa na kwamba zaidi ya Asilimia 80 walikuwa ni akina Mama. Nawapongeza Viongozi wa Viwanda hivi kwa jitihada ambazo wanazifanya kuendeleza uzalishaji na hivyo kuchangia Mapato kwa Serikali na Ajira kwa Wananchi.

Mheshimiwa Spika,
49. Kiwanda cha Sunflag ni Kiwanda pekee Nchini kinachozalisha nguo kuanzia hatua ya Pamba kutoka kwa Mkulima hadi nguo za kuvaa. Sunflag wamekuwa ni Soko zuri na la uhakika la Pamba ya Wakulima. Nawapongeza kwa uamuzi wao huo ambao una faida kubwa kwa Wakulima wa Pamba. Viongozi wa Viwanda hivyo walinieleza changamoto mbalimbali wanazokabiliana nazo. Serikali itafanya kila lililo ndani ya uwezo wake kuimarisha Viwanda vinavyotumia pamba ya Tanzania na kuweka mazingira yatakayoendelea kuvutia uwekezaji katika Sekta hii ya Nguo na Mavazi. Baada ya kupata taarifa ya Timu niliyoitaja hapo awali, Serikali itachukua hatua zitakazoondoa changamoto zinazovikabili Viwanda vya Nguo na Mavazi Nchini.

Mheshimiwa Spika,
50. Katika Kiwanda cha Minjingu Mines and Fertilizer Limited nilielezwa kuwa wamefanikiwa kuzalisha mbolea ya Minjingu Mazao ambayo ni bora kuliko Mbolea aina ya DAP kwa kuwa ina virutubisho vya Nitrogen, Phosphorous, Sulphur, Calcium na rutuba kama Magnesium, Zinc na Boroni. Aidha, Minjingu Mazao ina bei ndogo kuliko DAP. Kiwanda kwa sasa kina akiba (stock) ya Tani 5,600 ya Phosphate na Tani 7,100 ya Minjingu Mazao. Nilielezwa kuwa matumizi ya Mbolea ya Minjingu Nchini yamekuwa yakipungua mwaka hadi mwaka kutokana na matatizo mbalimbali ikiwemo hujuma inayofanywa kwenye Mfumo wa Ruzuku za Pembejeo. Napenda kuhimiza Wizara ya Kilimo, Chakula na Ushirika ione namna ya kukikwamua Kiwanda cha Minjingu kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu – TAMISEMI ili kuongeza matumizi ya mbolea za Minjingu.

SENSA YA WATU NA MAKAZI YA MWAKA 2012

Mheshimiwa Spika,
51. Itakumbukwa kuwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati akitoa hotuba yake ya kumaliza mwaka 2011 alitangaza rasmi dhamira ya Serikali kufanya Sensa ya Watu na Makazi ambayo imepangwa kufanyika Nchini kote tarehe 26 Agosti 2012. Mheshimiwa Rais alisisitiza kuwa Sensa ya Watu na Makazi pamoja na Vitambulisho vya Taifa ni mojawapo ya vipaumbele vya Taifa kwa mwaka huu wa 2012. Tarehe 12 Aprili 2012, Waheshimiwa Wabunge walipata fursa ya kuhudhuria Semina kuhusu Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2012. Katika Semina hiyo yalitolewa maelezo ya kina kuhusu hatua iliyofikiwa katika maandalizi ya Sensa ya Watu na Makazi. Nina imani kuwa baada ya Semina hiyo ya tarehe 12 Aprili 2012, hivi sasa Waheshimiwa Wabunge wana uelewa mpana kuhusu umuhimu wa taarifa zitokanazo na Sensa na kwamba watatumia uelewa huo kuwaelimisha Wananchi umuhimu wa kujiandikisha.

Mheshimiwa Spika,
52. Sensa ya Watu na Makazi ya mwaka 2012 madhumuni yake makubwa ni kupata takwimu kuhusiana na idadi ya Watu na kukusanya Taarifa za kina za Kiuchumi, Kijamii na Maelezo ya Makazi. Taarifa hizi hutumiwa na Serikali na Taasisi nyingine kwa shughuli mbalimbali za Mipango na maendeleo. Serikali pia hutumia Takwimu zitokanazo na Sensa katika kutunga Sera, kufanya maamuzi juu ya Utawala wa Umma kwa kuzingatia mahitaji halisi na vigezo vingine kama vile umri, jinsia na vinginevyo.

Mheshiwiwa Spika,
53. Sensa ya mwaka 2012 ina umuhimu wa kipekee kwa kuwa taarifa zitakazokusanywa zitatumika kufuatilia na kutathmini utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo ya Mwaka 2025 kwa Tanzania Bara na mwaka 2020 kwa Tanzania Zanzibar. Vilevile, taarifa hizo zitatumika kutathmini Mkakati wa Kukuza na Kupunguza Umaskini Tanzania Bara (MKUKUTA) na Mkakati wa Kupunguza Umaskini Tanzania Zanzibar (MKUZA). Takwimu hizo zitatumika pia kutathmini utekelezaji wa Malengo ya Milenia ifikapo mwaka 2015; Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano wa
2011/2012 – 2015/2016 pamoja na kubuni mikakati ya utekelezaji wa Mpango Elekezi wa Miaka 15 wa Utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo hadi mwaka 2025.

Mheshimiwa Spika,
54. Pamoja na maandalizi yanayoendelea hivi sasa, mafanikio ya Sensa yatategemea sana ushiriki wa Umma na Wadau wengine. Sisi Waheshimiwa Wabunge ni Wajumbe wa Kamati za Sensa za Wilaya na Halmashauri zetu na moja ya majukumu ya Kamati hizo ni kuhamasisha na kuelimisha Umma kuhusu umuhimu wa Sensa ya Watu na Makazi ili kuhakikisha kuwa kila mtu atakayelala Nchini Usiku wa Kuamkiasiku ya Sensa, yaani tarehe 25 Agosti 2012 kuamkia tarehe 26 Agosti 2012, anahesabiwa, na kwamba anahesabiwa mara moja tu.

Mheshimiwa Spika,
55. Zoezihili ni la Kitaifa hivyo linahitaji uhamasishaji na ushirikishwaji wa Wananchi wote. Natoa wito kwa Wananchi wote kushiriki kikamilifu katika zoezi la Sensa ya Watu na Makazi na kutoa ushirikiano mkubwa kwa Makarani wa Sensa watakaofanya kazi ya Kuhesabu Watu siku ya tarehe 26 Agosti 2012. Vilevile, naomba nitumie fursa hii kuwaomba Waheshimiwa Wabunge washirikiane na Viongozi wengine kusimamia utekelezaji wa shughuli zote za Sensa katika Wilaya na Halmashauri kwa kuhakikisha kuwa elimu kwa Wananchi inatolewa. Nawaomba pia Waheshimiwa Wabunge kutumia nafasi zao kama Wawakilishi wa Wananchi kuhamasisha na kuelimisha Umma kuhusu umuhimu wa kushirikiana na Makarani wa Sensa wakati wa kipindi cha kuhesabu Watu kwa kutoa Takwimu sahihi na hivyo kupata taarifa sahihi kwa ajili ya Mipango endelevu ya maendeleo. Kaulimbiu yetu kila wakati iwe ni Sensa kwa Maendeleo ya Taifa: Jiandae Kuhesabiwa. Napenda kuwatakia mafanikio mema katika kazi hii muhimu kwa Taifa letu.

MPANGO WA KUTOA KIFUTA MACHOZI CHA MIFUGO

Mheshimiwa Spika,
56. Mwaka 2008/2009, Mikoa ya Kaskazini hasa Mikoa ya Arusha na Manyara ilikumbwa na ukame mkubwa ambao ulisababisha Vifo kwa Mifugo. Kutokana na ukubwa wa tatizo hilo, Mheshimiwa Rais aliahidi kutoa Kifuta Machozi kwa

kuwapatia Mifugo ya Mbegu Wafugaji waliopoteza Mifugo yao yote katika Wilaya za Longido, Monduli na Ngorongoro. Katika kutekeleza Ahadi ya Rais, Serikali iliunda Kikosi Kazi ambacho kilibaini kuwepo kwa Vifo vya Ng’ombe 403,839;Mbuzi 211,201 na Kondoo 121,118 katika Wilaya hizo. Vilevile, Kikosi Kazi kilibaini kwamba jumla ya Kaya 6,127katika Wilaya hizo zilipoteza Mifugo kutokana na ukame. Wilaya ya Longido ilikuwa na jumla ya Kaya 2,852;Monduli Kaya 1,484 na Ngorongoro Kaya 1,791 zilizoathirika na ukame ulioambatana na Vifo na Mifugo.

Mheshimiwa Spika,
57. Katika mwaka 2011/2012, Serikali ilitoa Tamko Bungeni kuhusu kutekeleza ahadi ya kutoa Kifuta Machozi kama mbegu (seed stock) kwa Kaya zilizopoteza Mifugo yote ili ziweze kurudi katika hali yao ya awali kama Wafugaji. Aidha, Mradi maalum ulianzishwa kwa ajili ya kununua Mifugo (Ng’ombe na Mbuzi) kwa ajili ya Wilaya husika. Ununuzi wa Mifugo hiyo utafanyika katika ngazi ya Halmashauri za Wilaya kwa kuzingatia Sheria ya Manunuzi Na. 21 ya mwaka 2004.

Mheshimiwa Spika,
58. Kufuatia kuundwa kwa Kamati mbalimbali (Mkoa, Halmashauri, Kata na Vijiji za kusimamia utekelezaji wa Mpango wa Kusambaza Mifugo ya Kifuta Machozi, Halmashauri za Wilaya zilielekezwa kutangaza zabuni za kuwapata wanunuzi wa Mifugo ndani ya maeneo ya Wilaya husika katika kipindi cha Siku Tisini (90). Utekelezaji wa Zoezi hili utafanyika kwa Awamu kulingana na upatikanaji wa fedha. Aidha, Awamu ya Kwanza itaanza kwa kununua Ng’ombe 500 kwa kila Wilaya. Lengo ni kukamilisha zoezi hili kabla ya Kiangazi kuanza.

Mheshimiwa Spika,
59. Napenda kulijulisha Bunge lako Tukufu kuwa Uzinduzi wa Mpango wa kutoa Kifuta Machozi ulifanywa na Mheshimiwa Rais, Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete tarehe 19 Februari 2012 katika Wilaya ya Longido ambapo Serikali ilitumia Shilingi Milioni 213 kwa kununua na kusambaza Ng’ombe 500.

60. Aidha, ununuzi wa Mifugo kwa ajili ya Wilaya za Monduli na Ngorongoro utakamilika mara Serikali itakapokamilisha taratibu za kutuma fedha kwa Halmashauri za Wilaya hizo. Kiasi cha Shilingi Milioni 206 zimetengwa kwa ajili ya Wilaya ya Monduli na Shilingi Milioni 218 kwa ajili ya Wilaya ya Ngorongoro ili kuwezesha ununuzi wa Ng’ombe 500 kwa kila Wilaya.

61. Matumaini yangu ni kuwa zoezi la kutoa Kifuta Machozi kwa Wananchi wa Wilaya za Monduli na Ngorongoro litakamilika katika muda mfupi ujao kwa kuwa Mifugo hiyo ipo tayari kwa Wazabuni. Kinachosubiriwa ni malipo ya fedha. Natoa wito kwa Wafugaji na Wananchi walioathirika na ukame ambao wanasubiri Awamu ya Pili kuwa na subira wakati Serikali inatafuta fedha za kutekeleza Mpango huu.

HITIMISHO

Mheshimiwa Spika,
62. Kabla ya kuhitimisha hotuba yangu, napenda kusisitiza maeneo muhimu yafuatayo:

Kwanza: Tumeanza Mchakato wa Utekelezaji wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba. Mchakato ambao ni Msingi wa Utawala Bora. Natoa wito kwamba, Tuwaelimishe Wananchi kuhusu Mambo ya Msingi wakati wa kuchangia Maoni, na kwamba Mabadiliko ya Katiba siyo Mchakato wa kuwepo au kutokuwepo kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Pili: Tunayo Mifuko ya Hifadhi ya Jamii ambayo tukiitumia vizuri, ni kinga na kichocheo muhimu cha Kuondoa Umaskini na Kukuza Uchumi. Tushirikiane na Mamlaka ya Hifadhi ya Jamii kuwaelimisha Wananchi kuhusu umuhimu wa kujiunga na Mifuko ya Hifadhi ya Jamii kwa faida yao, kwani hivi sasa haijalishi kama uko kwenye Sekta Rasmi au Isiyo Rasmi.

Tatu: Bado tunazo changamoto nyingi katika Sekta ya Elimu, hasa katika Miundombinu na Ubora wa Elimu kwa ujumla. Tushirikiane katika kutekeleza Mikakati ya kutuwezesha kuwa na Elimu Bora kwa Watoto wetu. Tuwajengee utamaduni wa kujiamini na kushiriki kikamilifu katika kuboresha Miundombinu muhimu kuanzia Shule za Msingi, Sekondari hadi Vyuo.

Nne: Kuwepo kwa Viwanda Nchini ni muhimu kwa maendeleo yetu na Uchumi wa Nchi. Pamoja na changamoto zilizopo ni vizuri kuweka umuhimu wa kutumia bidhaa zinazozalishwa na Viwanda vyetu.
Tano: Tarehe 26 Agosti 2012 itakuwa ni Siku ya Sensa ya Watu na Makazi Nchini. Tuwahamasishe Wananchi waelewe umuhimu wa kuhesabiwa siku hiyo na utaratibu utakaotumika ikiwa ni pamoja na kila Mtu kuhakikisha anahesabiwa na kwamba anahesabiwa mara moja tu.

Mheshimiwa Spika,
63. Tunapohitimisha Mkutano huu wa Saba, pamoja na kumshukuru Mwenyezi Mungu tunao wajibu wa kiungwana kuwashukuru pia wote walioshiriki katika kutoa huduma muhimu katika kufanikisha Mkutano huu. Nitumie fursa hii kutoa shukrani za dhati kwako wewe Mheshimiwa Spika kwa kutuongoza vizuri na hatimaye kukamilisha Vikao vyote kama ilivyopangwa. Vilevile, namshukuru Naibu Spika pamoja na Wenyeviti wa Bunge kwa kazi nzuri. Niruhusu nimshukuru Dkt. Thomas Kashilillah, Katibu wa Bunge na Wasaidizi wake kwa kutuwezesha kufanya kazi hii kwa ufanisi mkubwa. Niwashukuru pia Wataalam wote ambao mchango wao kwetu umekuwa ni muhimu sana. Niwashukuru Askari, Madereva, Wanahabari kwa kushiriki kikamilifu katika kufanikisha Mkutano huu.

Mheshimiwa Spika,
64. Leo tunapohitimisha Mkutano huu wa Saba, tunapata fursa ya kujiandaa kwa ajili ya Mkutano wa Nane ambao ni Mahsusi kwa ajili ya Bajeti ya Mwaka 2012/2013. Napenda kuwatakia maandalizi mema kwa ajili ya Bajeti ya Serikali. Ni dhahiri kwamba bado tuna changamoto nyingi. Nawasihi kila mmoja wetu kujiwekea malengo ya kutimiza wajibu wake katika kufikia yale yote tunayoyatarajia kuyafanya kwa ajili ya Maendeleo ya Nchi yetu. Nimalizie kwa kuwatakia nyote safari njema ya kurejea katika maeneo yenu ya kazi.

Mheshimiwa Spika,
65. Baada ya kusema haya, naomba kutoa hoja kwamba Bunge lako Tukufu liahirishwe hadi tarehe 12 Juni 2012 Saa 3:00 Asubuhi, litakapokutana kwenye Ukumbi huu hapa Mjini Dodoma kujadili Bajeti ya Serikali.

66. Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja.